Picha : KAMPENI NYUMBA NI CHOO YAZINDULIWA SHINYANGA, WANASIASA WANYOOSHEWA KIDOLE


Kampeni ya kuhamasisha wananchi wa mkoa wa Shinyanga kuwa na vyoo kwenye nyumba zao "Nyumba ni Choo", imezinduliwa na mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe.Zainab Telack, na kuwaonya wanasiasa ambao watawakingia kifua wananchi ambao watachukuliwa hatua kwa sababu ya kutokuwa na vyoo kwenye kaya zao kwa madai ni wapiga kura wao, kuwa atakaye fanya hivyo atashughulikiwa.


Kampeni hiyo ambayo itadumu ndani ya siku 21 imezinduliwa rasmi leo Septemba 3,2019 kwenye viwanja vya Zimamoto Mjini Shinyanga  na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, mashirika, na wanasiasa.

Akizindua kampeni ya 'Nyumba ni Choo', Telack amewaagiza maofisa afya wote wa mitaa kupeleka mipango kazi yao, ili waweze kupita kila Kaya za mkoa huo na kuzikagua nyumba ambazo hazina vyoo,na kuwachukulia hatua wahusika lengo likiwa ni kuhakikisha kaya zote ziwe na choo bora.

Amesema anatambua kipindi hiki ni cha kuelekea kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa, hivyo wakati zoezi hilo la ukaguzi wa choo kwa kila nyumba likiendelea wanasiasa wanapaswa kutoliingilia, na kuanza kuzuia wananchi wasiwajibishwe kwa madai ni wapiga kura wao.

“Kwenye kampeni hii ya nyumba ni choo hatutaki siasa, bali tunataka wananchi waishi salama wawe na vyoo bora kwenye nyumba zao, hivyo Mwanasiasa ambaye atamkingia kifua mwananchi ambaye atakutwa hana choo nipeni taarifa ili tuone namna ya kumshughulikia, hatutaki mzaa kwenye masuala ya maendeleo,” amesema Telack.

“Hadi kufikia Desemba mwaka huu tunataka mkoa wetu, kaya zote ziwe na vyoo bora pamoja na kuvitumia, na kuondokana pia na dhana potofu ya kujisaidia vichakani kwa kuongopa kuchangia choo kimoja na mama mkwe, bali tunataka mkoa uwe safi kimazingira na wananachi wawe salama kiafya,” ameongeza.

Naye Afisa Afya wa mkoa wa Shinyanga Neema Simba, ametaja takwimu za kaya zenye vyoo mkoani humo kuwa ni asilimia 50.6 na kaya ambazo hazina vyoo ni asilimia 5.5 ambapo jumla ya kaya zote zipo 284,701.


Kwa upande wake mratibu wa uhamasishaji wa kampeni hiyo kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Elizabeth Malingumu amesema wamezindua kampeni ya nyumba ni choo mkoani Shinyanga, ili wananchi wote wawe na vyoo bora ili waepukane na magonjwa ya mlipuko na kuishi salama.


TAZAMA MATUKIO KATIKA PICHA HAPA CHINI


Mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Mhe. Zainabu Telack akizindua Kampeni ya nyumba ni choo na kuwataka wananchi wa mkoa huo wa Shinyanga kujenga vyoo bora pamoja na kuvitumia. Picha zote na Marco Maduhu - Malunde1 blog

Mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Mhe. Zainab Telack akitoa onyo kwa wanasiasa kuingilia oparesheni ya ukaguzi wa choo kwa kila nyumba na kuwakingia kifua wale ambao watakutwa hawana vyoo kwa madai ni wapiga kura wao.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Mhe. Jasinta Mboneko, akizungumza akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni ya Nyumba ni choo ambapo amesema wataisimamia na kuhakikisha inafanikiwa kwa wananchi wote kuwa na vyoo bora.

Awali Afisa Afya wa mkoa wa Shinyanga Neema Simba akisoma taarifa ya usafi wa mazingira ya mkoa wa Shinyanga. ametaja Takwimu kuwa kati ya kaya za mkoa wa Shinyanga 284,701 wanaotumia vyoo ni asilimia 50.6 na wasio na vyoo ni asilimia 5.5.

Mratibu wa uhamasishaji wa kampeni hiyo kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Elizabeth Malingumu akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni ya Nyumba ni choo. Amesema wamezindua kampeni hiyo ili kuhamasisha wananchi wote wa mkoa wa Shinyanga wanakuwa na vyoo bora kwenye nyumba zao.

Mwakilishi kutoka Shirika la Maendeleo la uholanzi (SNV) Elisekile Bwile, akielezea namna wanavyosaidiana na Serikali kuhakikisha nchi ya Tanzania wananchi wake wanakuwa kwenye mazingira ya usafi pamoja na kufadhili kujenga miradi ya kuhifadhia maji taka ukiwamo na mji wa Shinyanga.

Balozi wa kampeni ya nyumba ni choo msanii Mrisho Mpoto akizungumza na wananchi wa mkoa wa Shinyanga na kuwataka wajenge vyoo bora, vilivyoezekwa mapaa juu, milango pamoja na kuwepo na maji ya kunawa mikono.

Diwani wa Kata ya Kambarage manispaa ya Shinyanga Hassan Mwendapole akizungumza kwenye uzinduzi wa kampeni hiyo ya nyumba ni choo.

Awali Katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga Albert Msovela, akizungumza kwenye uzinduzi wa kampeni hiyo ya nyumba ni choo, kabla ya kuanza kutambulisha viongozi mbalimbali wa Serikali.

Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack katikati, akiwa na mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko (wa kwanza kushoto), pamoja na katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga Albert Msovela kabla ya kuzindua kampeni hiyo ya nyumba ni choo.

Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack awali kabla ya kwenda kwenye viwanja vya Zimamoto kuzindua kampeni ya nyumba ni choo akipiga picha ya pamoja na Balozi wa uhamasishaji wa kampeni hiyo Mrisho Mpoto kwenye ofisi ya mkuu wa mkoa.

Wananchi wa Shinyanga mjini wakiwa kwenye uzinduzi wa kampeni ya nyumba ni choo na kutakiwa wale ambao hawana vyoo, wajenge vyoo bora pamoja na kuvitumia ili waweze kujikinga na magonjwa mbalimbali ya mlipuko kikiwamo kipindupindu.

Wananchi wa Shinyanga mjini wakiwa kwenye uzinduzi wa kampeni ya nyumba ni choo na kutakiwa wale ambao hawana vyoo, wajenge vyoo bora pamoja na kuvitumia ili waweze kujikinga na magonjwa mbalimbali ya mlipuko kikiwamo kipindupindu.

Wananchi wa Shinyanga mjini wakiwa kwenye uzinduzi wa kampeni ya nyumba ni choo na kutakiwa wale ambao hawana vyoo, wajenge vyoo bora pamoja na kuvitumia ili waweze kujikinga na magonjwa mbalimbali ya mlipuko kikiwamo kipindupindu.

Wananchi wa Shinyanga mjini wakiwa kwenye uzinduzi wa kampeni ya nyumba ni choo na kutakiwa wale ambao hawana vyoo, wajenge vyoo bora pamoja na kuvitumia ili waweze kujikinga na magonjwa mbalimbali ya mlipuko kikiwamo kipindupindu.

Wananchi wa Shinyanga mjini wakiwa kwenye uzinduzi wa kampeni ya nyumba ni choo na kutakiwa wale ambao hawana vyoo, wajenge vyoo bora pamoja na kuvitumia ili waweze kujikinga na magonjwa mbalimbali ya mlipuko kikiwamo kipindupindu.

Mkurugenzi wa manispaa ya Shinyanga Geofrey Mwangulumbi (kushoto), akiwa na mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Hoja Mahimba, wakishuhudia uzinduzi wa Kampeni ya nyumba ni choo, ya kuhamasisha wananchi wawe na vyoo bora kwenye nyumba zao.

Viongozi mbalimbali wa kiserikali pamoja na vyombo vya dola, wakifurahia jambo kwenye uzinduzi huo wa Kampeni ya Nyumba ni choo mkoani Shinyanga, ya kuhamasisha wananchi wajenge vyoo bora pamoja na kuvitumia.

Burudani zikitolewa kwenye uzinduzi wa kampeni hiyo ya nyumba ni choo mkoani Shinyanga.

Burudani zikiendelea kutolewa.

Burudani zikiendelea kutolewa.

Burudani zikiendelea kutolewa kwenye uzinduzi wa kampeni ya nyumba ni choo.

Awali Mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Mhe. Zainabu Telack, wa pili kutoka kushoto, akiwa na mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akifuatiwa na Katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga Albert Msovela, pamoja na Mrisho Mpoto wa kwanza kushoto, akiongoza maandamano kwenda kuzindua kampeni ya nyumba ni choo.

Waendesha Bodaboda wakiwa kwenye maandamano ya kwenda kuzindua kampeni ya nyumba ni choo, kwenye viwanja vya Zimamoto Shinyanga Mjini, kwa kuhamasisha wananchi wa mkoa wa Shinyanga wawe na vyoo bora pamoja na kuvitumia.


Picha zote  na Marco Maduhu- Malunde 1 Blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527