Bashe Abaini Ufisadi Wa Bilioni 10 Bodi Ya Korosho

Naibu Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe  ameiagiza Bodi ya Korosho nchini kuhakikisha shilingi bilioni 10 kutoka hazina zilizotolewa kwa ajili ya kununua mbolea na viwatilifu kwenye zao la korosho zinarudi hazina, baada ya bodi hiyo kuzitumia kinyume na maelekezo ya serikali.

Naibu Waziri Bashe aliyasema hayo katika ziara yake ya kukagua kontena zaidi ya 350 za mbolea na viatilifu yaliyopo katika bandari kavu tatu ikiwamo ya Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) na Azam za jijini Dar es Salaam.

"Kuna kampuni inaitwa Bajuta imepewa bilioni 4.5 kati ya bilioni 10 na Bodi ya Korosho zilizotolewa na hazina kwenda kwa Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC), wakati Bodi ya korosho inafanya maamuzi hayo hayakuwa ni maamuzi ya serikali"- Alisema Bashe na kuongeza;

"Naagiza  ufanyike ukaguzi maalum na ukaguzi wa uwezo kwa kampuni ya pembejeo na viwatilifu ya Bajuta, juu ya mnyororo wa usambazaji pamoja na usambazaji wa pembejeo katika sekta ya kilimo na ukaguzi huo usifanywe na Wizara ya kilimo Bali ufanywe na hazina ili viongozi wote waliobadilisha matumizi ya Sh. bilioni 10 zilizoelekezwa kwenda Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) wachukuliwe hatua  mara moja."

Akifafanua alisema TFC ilipewa jukumu la kuagiza mbolea na dawa aina ya Salfa ili iweze kuuzwa kwa wakulima kwa bei nafuu, lakini ilipokea Sh. bilioni moja kati ya 10 iliyotolewa na Hazina na hivyo bodi hiyo kuwakwamisha kutimiza malengo ya serikali.

Alisema mwaka mmoja sasa TFC, bandari kavu hizo zinashikilia kontena zaidi ya 350 zenye mbolea na Salfa.
 
"Rais Dk. John Magufuli alipotoa fedha hizo kwenda TFC alikusudia wakulima wapate unafuu wa mbolea na viatilifu ili kuwaboreshea kilimo chao, nasisitiza kwamba Kampuni ya Bajuta irudishe Sh. bilioni 4.5 mali ya serikali," alisema Bashe.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments