WAJUMBE BARAZA LA WAZAZI WA CCM WAHAMASISHWA KUJIUNGA NA BIMA YA AFYA

Na Editha Karlo- Malunde 1 blog

Meneja wa bima ya afya (NHIF)Mkoa wa Geita Elias Odhiambo amewashauri wajumbe wa baraza la Jumuiya ya Wazazi ya CCM wilaya ya Chato kujiunga na bima ya afya  ili kuwa na uhakika wa matibabu wanapougua wao na familia zao.


Akizungumza leo kwenye kikao cha Jumuiya hiyo katika ukumbi wa CCM Wilaya ya Chato,Othiambo amewahamasisha wajumbe wa Baraza la Jumuiya ya wazazi wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) wilaya ya Chato  kujiunga na Bima ya Afyaili kuwa na uhakika wa kupata matibabu na dawa pale wanapougua hata kama hawana pesa mfukoni. 

"Ugonjwa huwa unakuja bila ya taarifa,unaweza kuugua mfukoni huna hata pesa,lakini unapokuwa na kadi yako ya bima ya afya unakuwa na uhakika wa kupata matibabu na dawa",alisema Odhiambo.

"Mkiwa kama wasimamizi wa ilani ya chama tawala, niwaombe mjiunge na utaratibu wa Bima ya Afya, kwani sasa wananchi wana wigo mpana wa kujiunga na Bima ya afya kupitia NHIF au CHF iliyoboreshwa",alisema Meneja

Alisema upande wa NHIF zipo huduma mbalimbali za bima kama Bima kwa watumishi, Ushirika Afya kwa Wakulima, Bima  kwa Watoto na Wanafunzi,Vile vile hivi karibuni NHIF itaanzisha mpango wa Bima ya Afya kwa mtu mmoja mmoja.

Odhiambo alisema kujiunga na Bima ya Afya ni kuwekeza kwenye afya yako ili kukabiliana na changamoto ya ugonjwa kuja bila hodi na kujikuta unatumia gharama kubwa kupata matibabu. 

 Amewaomba kutimiza wajibu hao kupitia kauli yao ya uchungu wa mwana aujuaye  mzazi kwa kujiunga na Bima ya afya sambamba wananchi wengine kujiunga na Bima ya afya.

Akielezea jinsi ambavyo yeye na familia yake wamekuwa wanufaika wa NHIF, Katibu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Wilaya ya Chato Acheny Mwinshehe Maulidi ameahidi kuwa balozi wa kuhamasisha wananchi kujiunga na bima ya afya.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527