MAMA WA KAMBO MBARONI KWA TUHUMA YA KUUA MTOTO SHINYANGA


Kamanda wa Polisi mkoa wa Shinyanga,ACP Richard Abwao
Jeshi la Polisi mkoani Shinyanga linamshikilia Mwanamke aitwaye Fotuna Jackson, Mkazi wa Kitangiri Manispaa ya Shinyanga kwa tuhuma za mauaji ya mtoto wake wa kambo mwenye umri wa miaka miwili.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Richard Abwao, amesema Mwanamke huyo anatuhumiwa kumpiga mara kwa mara mtoto na kwa mujibu wa uchunguzi wa Daktari umethibitisha kuwa kipigo kilisababisha kuvia damu katika mgongo wa mtoto na kusababisha kifo chake.

"Fotuna alikuwa akiishi na mtoto huyo mwenye umri wa miaka miwili ambaye siyo mtoto wake wa kumzaa,Juzi alikuwa amempeleka kituo cha afya Chamaguha wakati anaugua,yule mtoto alifariki dunia na walivyoenda kupima wakagundua kwamba alikuwa amepigwa,sehemu za mgongoni zilikuwa na hali ya kuvia damu ambapo baada ya uchunguzi wa Daktari ulithibisha kuwa kile kipigo kilisababisha kifo cha mtoto huyo",ameeleza Kamanda Abwao.

"Kuna tuhuma zinaelezwa kuwa mama huyo alikuwa anampiga mara kwa mara mtoto huyo,na hata mwili wa mtoto huyo ulikutwa na makovu kuonesha kuwa huyo mtoto alikuwa anaadhibiwa kwa kiwango kikubwa kuliko kawaida ya malezi ya mtoto",amesema Kamanda Abwao

Kamanda Abwao amesema upelelezi unaendelea na ukikamilika mtuhumiwa atapelekwa mahakamani.
Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527