WAZIRI WA KILIMO AUTAKA UONGOZI WA MKOA WA SIMIYU KUANZA HARAKA UTEKELEZAJI WA BIMA YA MAZAO

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Simiyu
Uongozi wa Mkoa wa Simiyu umetakiwa kuanza haraka utekelezaji wa mkakati kabambe uliozinduliwa leo tarehe 3 Agosti 2019 na Waziri wa Kilimo kuhusu Bima ya Mazao kwa wakulima.


Waziri Hasunga ameyasema hayo wakati wa kikao kazi kilichofanyika katika ukumbi wa mkuu wa mkoa wa Simiyu na kuhudhuriwa na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa huo kupokea maelekezo yaliyotolewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Kassim Majaliwa kuhusu mustakali wa zao la Pamba.

Mhe Hasunga alisema kuwa kuanza haraka kwa utekelezaji wa uandikishaji wa wakulima kutaimarisha uwezekano wa kuboresha maisha ya wakulima ambao katika kipindi kirefu wameumia kupitia majanga mbalimbali wanayokumbana nayo ikiwemo mazao yao kuungua moto ama ukame.

Alisema kuwa uzinduzi wa Bima ya Mazao umefanyika katika mkoa wa Simiyu hivyo mkoa huo unapaswa kuanzisha haraka utekelezaji wake.

Katika kikao hicho Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe Antony Mtaka amempongeza Waziri wa Kilimo kwa kipindi cha muda mfupi ameweza kuonyesha dira na muelekeo chanya katika ukombozi wa sekta ya kilimo nchini.

Alisema kuwa maamuzi ya wizara ya kilimo inayosimamiwa na Mhe Hasunga ya kuanzisha Bima ya Afya, na Usajili wa wakulima ni miongoni mwa mambo muhimu yatakayoinua sekta ya kilimo nchini.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527