WAZIRI MKUU: MSIMU UJAO MALIPO YA WAKULIMA WA PAMBA YAPITIE BENKI


WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa ameagiza kwamba kuanzia mwakani malipo yote ya wakulima wa pamba yawe yanapitia benki ambapo wakulima wataingiziwa fedha kupitia akaunti zao.

Hivyo, ametumia fursa hiyo kuwasihi wakulima wafungue akaunti katika benki mbalimbali zilizopo kwenye maeneo yao ili waweze  kufanikisha mkakati huo na pia kuhifadhi fedha zao kwa ajili ya matumizi ya baadae.

Waziri Mkuu alitoa agizo hilo jana jioni (Alhamisi, Agosti 8, 2019) wakati akizungumza na wananchi wa kijiji cha Luguru, wilayani Itilima mara baada ya kukagua ghala la pamba la Chama cha  Ushirika cha Msingi cha  Maendeleo.

Alitembelea kijiji hicho kwa lengo la kujionea mwenendo wa uuzaji wa zao la pamba katika Chama cha Msingi Maendeleo na alihakikishiwa kwamba kwa sasa uuzaji wa pamba unaendelea vizuri

Waziri Mkuu alisema ni vizuri malipo ya wakulima yapitie benki ili kuwawezesha kupanga matumizi mazuri ya fedha zao na pia watapa fursa ya elimu ya matumizi mazuri ya fedha.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alieleza miradi mbalimbali inayotekelezwa na Serikali katika wilaya hiyo ukiwemo mradi wa ujenzi wa hospitali ya wilaya ambao umefikia asilimia 95.

“Jumla shilingi bilioni 1.5 zimetolewa na Serikali kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya wilaya inayojengwa eneo la Nguno, ambapo majengo yote saba ya kiupaumbele yamekamilika.”

Alisema mwaka 2017/2018 Serikali ilitoa sh. bilioni 2.34 kwa ajili ya miradi ya maji ya vijiji vya Lagangabilili, Mwamapalala, Kabale, Ikungulipu na Isengwa, yote imekamilika na inatoa maji.

Alisema mwaka 2019/2020 Halmashauri hiyo kupitia RUWASA imetengewa sh. bilioni 4.84 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya maji. Mradi huo utavinufaisha vijiji 78.

Awali,Katibu Mkuu wa Chama cha Msingi cha Maendeleo Luguru na Itubilo, Buzo Hussein alimshukuru Waziri Mkuu kwani wakati wote amekuwa mstari wa mbele katika kufuatilia kero mbalimbali zinazowakabili wakulima nchini na kuzitafutia ufumbuzi.

“Hii yote inatokana na kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli inayowataka viongozi kufuatilia changamoto za wananchi kwa vitendo na kuzitatua.”

Alisema katika ghala la chama chao kuna jumla ya kilo 175,235 za pamba ambazo zimekusanywa kutoka kwa wakulima ikiwa inasubiri wanunuzi.

 (mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527