WAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA KUFUNGUA KONGAMANO LA WADAU WA UWEKEZAJI KAGERA

Mkuu wa mkoa wa Kagera Brigedia Jenerali Elisha Marco Gaguti.


Na Lydia Lugakila - Malunde1 blog
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Kassim Majaliwa anatarajia kuzindua wiki ya uwekezaji mkoa wa Kagera Agosti 14 ,2019.


Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo Agosti 3, 2019, Mkuu wa mkoa wa Kagera Brigedia Jenerali Elisha Marco Gaguti akiwa kamati ya maandalizi ya wiki ya Kagera katika kikao kilichofanyika katika ofisi za mkoa huo zilizopo manispaa ya Bukoba,amewataka wananchi na wadau toka nje na ndani ya mkoa wa Kagera wakitakiwa kujitokeza kwa wingi  kushiriki katika wiki hiyo.

Mkuu huyo wa mkoa amewataka waandishi wa habari kupitia vyombo vyao vya habari kuwaalika wadau mbalimbali wa uwekezaji pamoja na wananchi wote wa nje na ndani ya mkoa wa Kagera kushiriki katika wiki ya uwekezaji Kagera.

"Ndugu wana habari wiki ya uwekezaji Kagera inatarajia kuanza Agosti 12, 2019, ambayo itaanza na maonyesho ya bidhaa au fursa  mbalimbali zinazopatikana  katika mkoa wa Kagera ambapo Tarehe 12-13/8/2019 na maonyesho hayo yatafanyika katika uwanja wa Gymkhana uliopo katika  Manispaa ya Bukoba",amesema.

Gaguti amesema Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa ndiye atafungua rasmi kongamano la wadau wa uwekezaji litakalofanyika katika ukumbi wa Hotel ya ELCT Bukoba.

Ameongeza kuwa tarehe 15 Agosti 2019 kongamano la wadau wa uwekezaji litaendelea ikiwa ni pamoja na maonyesho mbalimbali ambapo Agost 16 /2019 wiki ya uwekezaji itafungwa rasmi na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji Mh. Angela Kairuki na mara baada ya kufunga rasmi wadau wa uwekezaji watapata nafasi ya kwenda kutembelea vivutio vya Utalii pamoja na fursa za uwekezaji zilizomo mkoani Kagera hadi Agosti 17 mwaka huu.

Aidha Gaguti ameeleza kuwa wiki ya Kagera ni fulsa kwa wadau mbali mbali wa uwekezaji kuja Kagera kuwekeza hasa katika sekta za kilimo kutokana na misimu miwili ya mvua kwa mwaka lakini pia mazao mengi ya chakula na biashara yanakubalika sana katika mkoa huu akitolea mfano zao la ndizi, kahawa, vanilla, chai, kokoa na mazao ya chakula ni mahindi na maharage huku fursa nyingine zikiwa ni uvuvi, ufugaji, viwanda, elimu, utalii na utamaduni wa wananchi wa Bukoba.

Katika hilo ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi katika wiki hiyo ili kuufungua mkoa wa Kagera kimtaji na kiuchumi na kutengeneza ajira za vijana mkoani humo.

Pia Mkuu huyo wa Mkoa amezitaka taasisi zote za serikali na zisizokuwa za serikali zilizopo mkoani hapa kuhakikisha zinashiriki kikamilifu katika wiki ya uwekezaji ili kuonesha fursa walizonazo na kizitangaza kwa wadau mbali mbali ambao wanatarajia kuhudhuria katika wiki hiyo kutoka ndani na nje ya nchi.

Hata hiyo mkoa huo unatarajia kuwapokea mabalozi wanne kutoka nchi jirani za Congo, Kenya, Rwanda, Burundi, na Uganda sambamba na wafanyabiashara kutoka mataifa jirani ili waungane na wafanya biashara wa hapa ili kushirikiana kujenga uchumi endelevu, huku akitaja kauli mbiu ya wiki ya uwekezaji Kagera kuwa ni "Kagera: Eneo la kimkakati kwa uchumi wetu na Afrika Mashariki".

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527