Wakimbizi Wa Burundi Walalamika Kuzuiwa Na Mashirika Kurejea Nchini Kwao.... Waziri Lugola Aagiza Wakamatwe Wanaoweka Vikwazo

Na Felix Mwagara, Kibondo (MOHA).
Baadhi ya Wakimbizi kutoka nchini Burundi wanaoishi katika Kambi ya Nduta, Wilaya ya Kibondo mkoani Kigoma wamesema wanawekewa vikwazo na kucheleweshwa na baadhi ya watendaji wa mashirika ya wakimbizi kambini humo wakati wanapoomba kujiandikisha kurejeshwa kwao.

Wakizungumza katika mkutano wa hadhara ulioandaliwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola na Waziri wa Mambo ya Ndani na Elimu ya Uzalendo kutoka nchini Burundi, Pascal Barandagiye, wakimbizi hao wamesema wapo tayari kurudi nchini mwao kwa hiari lakini wanashindwa kujiandikisha kutokana na kukwamishwa na baadhi ya watendaji wa mashirika hayo.

Mkimbizi wa kambi hiyo, Nzoisa Bhainoje, alisema yupo tayari kurejea nchini Burundi lakini amefanya juhudi za kwenda eneo la kujiandikisha kambini hapo lakini hakufanikiwa kutokana na kusumbuliwa akiambiwa kuwa idadi wanaotakiwa kuondoka imekamilika.

“Nakumbuka nilifika eneo la kuondoka siku ya Jumanne lakini ilishindikana kujiandikisha kutokana na kukwamishwa, wengi tunataka kuondoka lakini tunashindwa kuondoka kwasababu tunakwamishwa,” alisema Bhainoje.

Bhainoje aliongeza kuwa, wanaomba watendaji hao wawaruhusu kwa wale wanaotaka kurejea nchini mwao kwa hiari, lakini kwa wale ambao hawataki kuondoka wanaweza kubaki kwa mipango yao.

Baada ya wakimbizi hao kutoa kero zao kwa Waziri Lugola na Waziri Barandagiye, ndipo Lugola aliagiza kufanyika uchunguzi katika kambi hiyo kuwakamata wale wote ambao wanakwamisha wakimbizi hao kurejea nchini kwao kwa hiari.

“Naagiza uchunguzi ufanyike haraka iwezekanavyo kwa yeyote atakayehusika anakwamisha zoezi hili la kuwarejesha wakimbizi hawa ambao wapo tayari kuondoka nchini kwao kutokana na amani iliyopo, awe Afisa kutoka Wizarani, awe afisa wa shirika lolote, awe yupo hapa kambini, lazima tutamkamata na kumpeleka mahakamani,” alisema Lugola.

Aliongeza kuwa, muda umefika kwa wakimbizi wa Burundi kurudi nchini mwao, kwasababu zile sababu ambazo zilikuwa zinazuia zoezi la kuwarudisha kwao wakimbizi hao kwa sasa havipo tena kwasababu nchi hiyo ina amani.

Alisema Serikali ya Tanzania chini ya Rais John Magufuli imejiridhisha sababu kubwa iliyowaleta wakimbizi hao wa Burundi nchini ya kutowepo kwa amani haipo tena na kwamba kwa sasa Burundi ipo salama kiulinzi na kiusalama pia kisiasa hivyo wakimbizi hao wanapaswa kurudi nchi mwao wote bila kuwepo kikwazo chochote.

“Wanaosema Burundi haina amani wanaipaka matope nchi hiyo kwani jambo hilo halina ukweli wowote na Tanzania imefanya uchunguzi wa kutosha na kujiridhisha kuwa amani ya kudumu ipo nchini humo, Oktoba Mosi tutaanza kutekeleza mkataba wa pande tatu wa kurudishwa kwa wakimbizi 2000 kila wiki wa Burundi kwenda nchini mwao”. Alisema Lugola.

Naye Waziri Barandagiye, kwa upande wake alisema Burundi iko tayari kutekelezwa kwa makubaliano ya pande tatu ya kuhakikisha wakimbizi wote wa Burundi wanaohifadhiwa kwenye makambi mbalimbali ya wakimbizi mkoani nchini wanarudi Burundi lakini wanashangazwa na namna Shirika la Kuhudumia Wakimbizi linavyoendesha zoezi hilo kwa kasi ndogo.

"Tuko tayari kupokea wakimbizi 3000 kila wiki zaidi ya takwimu ya wakimbizi 2000 iliyotolewa kwenye makubaliano ya pande tatu, maandalizi na matayarisho ya kupokea wakimbizi hao yapo vizuri na wengi wanaorudi wamekuwa wakipata misaada mbalimbali ikiwemo miradi ya kiuchumi kwa ajili ya kuendesha maisha yao,";Alisema Barandagiye.

Barandagiye amewataka wakimbizi hao kutokubali kudanyanywa na maneno ya wanasiasa kwamba hakuna amani nchini Burundi lakini kuwa na tamaa ya kwenda kuishi Marekaani, Canada kuwa huo ni uongo hivyo wanapaswa kurejea nchini mwao kwakuwa ipo amani na pia mazingira
yanaruhusu kuppokelewa.

Waziri Lugola na Barandagiye walitembelea Kambi ya Nduta, Wiliyani Kibondo na Mtendeli iliyopo Wilayani Kakonko mkoani humo, kwa lengo la kuhamasisha wakimbizi katika kambi hizo kurejea nchini kwao kwa hiari.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments