WAGANGA WAKUU WA MIKOA WATAKIWA KUSHIRIKIANA NA VIONGOZI WA VIJIJI KUHAKIKISHA KILA MWEZI WANAINGIZA KAYA MPYA 31 KATIKA CHF

Na.Faustine Gimu Galafoni,Dodoma.

NAIBU katibu mkuu ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI)anayeshughulikia Afya dokta DOROTHY GWAJIMA amewataka waganga wakuu wa mikoa kushirikiana na viongozi wa serikali za vijiji nchini kuhakikisha kila mwezi wanaingiza kaya mpya 31 za mfuko wa afya ya jamii iliyoboreshwa(CHF).

Dokta GWAJIMA amesema hayo alipotembelea Zahanati ya kijiji cha Chiboli wilayani Chamwino mkoani Dodoma kushuhudia namna ambavyo Zahanati hiyo imeweza kuandikisha idadi kubwa ya kaya katika mfumo huo.

Amesema zahanati hiyo ipo kijijini umbali wa km 90 lakini imeweza kuandikisha kaya 315 sawa na asilimia 63.

Azma ya serikali ni  kutengeneza mfumo wa bima ambao mwananchi atatambuliwa na pesa anayochangia itarudi kwenye kituo kama anavyoeleza meneja mradi wa HPSS Tuimarishe afya ALLY KEBBY.

Kwa upande wake mratibu wa CHF iliyoboreshwa mkoa FRANCIS LUTALALA amesema ili kupata mafanikio ni lazima uwepo ushirikiano baina ya viongozi.

Naye Muuguzi wa Zahanati hiyo SHIJA MAKEJA anaeleza siri kubwa ya mafanikio waliyoyapata kuwa  ni ushirikiano waliouweka baina yao na viongozi wa serikali ya kijiji.

Hadi kufikia agosti mwaka huu jumla ya kaya elfu 23,114 kati ya kaya laki 447,773 za mkoani hapa zimejiunga na CHF iliyoboreshwa huku uhamasishaji Zaidi ukiendelea kutolewa kwa kaya zote kuona umuhimu wa kujiunga na CHF iliyoboreshwa.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527