DKT. MWANJELWA : SERIKALI KUPITIA TASAF YAANDAA UTARATIBU MPYA WA KUWAPATA WALENGWA WA TASAF WENYE UFANISI ZAIDI


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb) akilakiwa na wananchi wa kijiji cha Burugo katika Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba Mkoani Kagera ambako yuko kwenye ziara ya kikazi kukagua utekelezaji
wa miradi ya TASAF na kukutana na Watumishi wa Umma kuhimiza uwajibikaji.
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb) akizungumza na wananchi  na Wanufaika wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini katika kijiji cha Burugo (hawapo pichani) juu ya utekelezaji wa miradi ya TASAF.
Baadhi ya Wananchi na Wanufaika wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini katika katika kijiji cha Lukindo kilichopo Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba Mkoani Kagera wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb) (hayupo pichani).
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa
(Mb) (katikati) akiwa nyumbani kwa mmoja wa walengwa wa TASAF katika kijiji cha Burugo Bi. Justa Migini (kulia kwa Naibu Waziri),wa kwanza kushoto ni Meneja wa
Miradi ya Ajira za Muda TASAF Bw. Paul Kijazi 
wakishuhudia nyumba iliyojengwa na mlengwa huyo kwa kutumia ruzuku ya TASAF.
Mmoja wa Wanufaika wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini wa kijiji cha Burugo, Halmashauri ya Wilaya ya
Bukoba Mkoani Kagera Bi. Agnes Kemilembe akitoa ushuhuda wa namna alivyotumia ruzuku kuboresha makazi yake kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya
Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb). Picha ya chini ni mlengwa huyo akimuonesha naibu waziri shamba lake analoliendeleza kwa
kutumia ruzuku ya TASAF. 

NA ESTOM SANGA---KAGERA 

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Dkt. Mary Mwanjelwa amesema Serikali kupitia TASAF imeandaa utaratibu utakaowezesha kuorodheshwa kwa walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini watakaokidhi vigezo vya umaskini. 

Akiwahutubia Wananchi na Walengwa wa TASAF katika vijiji vya Lukindo na Burugo katika halmashauri ya Wilaya ya Bukoba mkoani Kagera, Dkt. Mwanjelwa amesema utaratibu huo mpya wa kuzitambua na kuziorodhesha kaya za walengwa kwenye Mpango utahusisha matumizi ya kielektroniki na kupiga picha kwa wahusika ili kuondoa uwezekano wa kuorodhesha kaya zisizostahiki. 

Aidha Naibu Waziri huyo amesema serikali kupitia TASAF inaendelea kukamilisha maandalizi ya uzinduzi wa sehemu ya pili ya utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ambao amesema haitawapa mwanya wananchi wenye uwezo kujumuishwa kwenye Mpango huo. 

Amesema Walengwa wa Mpango huo wenye uwezo wa kufanya kazi watawekewa utaratibu wa kutekeleza miradi ya Maendeleo kwenye maeneo yao watakayoibua na kisha kulipwa ujira kama njia mojawapo ya kujiongezea kipato. 

Katika hatua nyingine Dkt. Mwanjelwa amewaagiza wataalamu wa sekta mbalimbali katika halmashauri za wilaya kutenga muda wa kuwatembelea Walengwa wa TASAF na kuona namna wanavyotekeleza miradi yao na kuwashauri namna bora zaidi ya kutekeleza miradi hiyo ili waweze kupata matokeo bora na yenye tija. 

Wakati huo huo ameonyesha kuridhishwa kwake na mafanikio waliyoanza kupata Walengwa wa TASAF katika Nyanja mbalimbali jambo linaloonyesha kuwa mkakati wa Serikali katika kupambana na umaskini unatekelezeka. 

Dkt. Mwanjelwa ameyasema hayo kwa nyakati tofauti alipotembelea vijiji vya Lukindo, na Burugo katika halmashauri ya Wilaya ya Bukoba Vijijini mkoani Kagera na kukutana na Walengwa ambako amekagua shughuli wanazozifanya kwa kutumia ruzuku wanayoipata kutoka TASAF. 

Naibu Waziri huyo amesema Walengwa hao wa TASAF wameweza kubadilisha maisha yao kwa kutumia ruzuku ya Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini kwa kuboresha maisha yao hususani katika Nyanja za makazi, uchumi huku wengine wakifanikiwa kujenga nyumba zao bora ikilinganishwa na hali ilivyokuwa kabla ya kupata ruzuku hiyo. 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527