SPIKA NDUGAI AIPIGIA CHAPUO UTALII WA FUKWE ZA PWANI YA BAHARI YA HINDI


SPIKA wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai ametoa wito kwa Serikali  kuendeleza utalii wa Pwani ya Bahari ya Hindi, hatua itakayosaidia kuchochea ukuaji wa  utalii nchini.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Jengo la tatu la abiria katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jana alhamisi (Agosti Mosi, 2019), Ndugai alisema Tanzania ina kila sababu ya kuendeleza fukwe hizo kutokana na ukweli kuwa Tanzania ina rasilimali nyingi za fukwe na bahari zilizo bora kuliko nchi yoyote ndani ya bara la Afrika.

Spika Ndugai aliongeza kuwa uendelezaji wa fukwe hizo  utasaidia nchi kwa kiasi kikubwa kupiga hatua na  kuifanya Tanzania kufikia uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.

“Sisi hapa Tanzania tuna pwani ya bahari nzuri zaidi kuliko pwani zingine popote pale Afrika, hizi ni hifadhi za mwambao wa Pwani ya Bahari ya Hindi, kuanzia Pangani mpaka Mtwara ambazo hazijatumika vizuri.” Alisema Spika Ndugai

Aidha Spika Ndugai aliongeza  fukwe hizo zikitumika vizuri zitasaidia kuongeza kiwango cha ukusanyaji wa mapato ya serikali kwa kuoanishwa vizuri kwa utalii wa pwani na ule wa bara na hivyo kuifanya sekta ya utalii kuongeza wigo mwingine wa mtandao wa mapato nchini.

Akizitaja sababu zilizopelekea utalii kutoonekana vizuri, Spika Ndugai alisema moja ya sababu kubwa inayochangia sekta ya  utalii  kutokufanyika vizuri ni kwa kuwa utalii wa fukwe za bahari bado uko chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Aidha katika kuonyesha umuhimu wa kuendeleza fukwe hizo, Ndugai aliyataja maeneo ya Mombasa, Lamu na Malindi nchini Kenya kama maeneo ambayo yamefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuendeleza fukwe katika Pwani zao, ambapo zimesaidia kuchochea ongezeko la watalii katika maeneo hayo.

“Kwenye Pwani zao kwa sasa kuna utalii maarufu unaofanyika baharini, unaofahamika kama ‘Marine Parks tourism’, ndio maana ukiangalia Pwani yao imejaa hotel, na sisi hapa kwetu tukitumia fukwe zetu vizuri tunaweza kuwa na utalii mzuri zaidi wa namna hii utakaosaidia kuongeza idadi ya watalii nchini”. Alisema Spika Ndugai.

Pia Spika Ndugai alimshukuru Rais Dkt. John Magufuli kwa kuamua kuipandisha hadhi iliyokuwa sehemu ya pori la akiba la Selous Game Reserve’ kuwa hifadhi kamili itakayojulikana kama Hifadhi ya Taifa ya Nyerere  au ‘Nyerere National Park’.

Akizungumzia kuhusu suala hilo Rais Magufuli alisema pendekezo la  kuendeleza fukwe  za pwani ya Bahari ya Hindi ni moja ya vipaumbele vya Serikali kwa sasa, na kumuagiza Waziri Mkuu , Kasim Majaliwa   kuangalia jinsi ya kuendeleza  fukwe zote kuanzia Moa hadi Msimbati.

MWISHO


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527