SERIKALI YATAJA SABABU YA NDEGE YA TANZANIA KUZUILIWA AFRIKA KUSINI


Msemaji wa Serikali, Dk Hassan Abbas amesema sababu ya kushikiliwa ndege ya Air Tanzania aina ya Airbus A200-300 ni kesi kati ya Serikali ya Tanzania na mkulima Hermanus raia wa Afrika Kusini ambaye mali zake zilitaifishwa.

Dk  Abbas amesema hukumu iliyotolewa na mahakama nchini Afrika Kusini inaruhusu kupinga hatua ya mahakama hiyo kuzuia ndege ya Air Tanzania, kwamba wanasheria watachambua kuona hatua za kuchukua.

Ameyasema hayo Jumapili Agosti 25, 2019 wakati akihojiwa na Shirika la Utangazaji nchini (TBC). 


“Niwakikishie Watanzania kuwa ndege zetu zipo salama ambazo zinaendeshwa na ATCL isipokuwa ndege hii moja iliyozuiliwa Afrika Kusini”

"Kesi hii ni madai ya muda mrefu ya fidia ya ardhi iliyotwaliwa tangu miaka ya 1980 huko, sio kesi kwamba ni ATCL ndiyo inadaiwa, tunaipambania ndege hii kwa maslahi ya Taifa letu na tunaamini siku moja itarudi kuendelea na shughuli zake za kawaida”

“Ni kesi ya fidia inayomuhusu Bwana Hermanus Steyn na Serikali ya Tanzania, kesi hii haina uhusiano wowote na Shirika letu la Ndege (ATCL), sisi tunaheshimu Sheria, Wanasheria wetu wanafuatilia na Sheria itafuata mkondo wake”

“Ukisoma hukumu inaturuhusu hata sisi kupinga, Wanasheria wetu wataichambua na kuona hatua gani za Kuchukua, tunawahakikishia Watanzania tutasimamia maslahi ya Taifa na ndege yetu itarudi na kuendelea na shughuli zake"

“Kesi ya msingi haijasikilizwa, kwa sababu ametumia Sheria za Afrika Kusini kuomba kutekeleza hukumu ya Nchi nyingine, ana hukumu ambayo ilishapatikana Nchini lakini akaomba itekelezwe Afrika Kusini kwa maana ya kiasi cha fedha kilichobaki”

“Kwenye awamu zote kulikuwa na makubaliano lakini ukifuatilia hatua za Kimahakama wanakubaliana lakini malipo hayafanyiki, kiasi kikubwa cha malipo kilifanyika katika awamu ya nne kikabaki kiasi kidogo ambacho ndio unaona amekwenda Afrika Kusini" amesema Dkt. Ababas.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527