SERIKALI KUPITIA UPYA SERA YA KILIMO ILI KUWANUFAISHA WAKULIMA


Serikali imesema  sera iliyopo ya sekta ya kilimo inayotumika sasa,  ndiyo cha chanzo cha wakulima kuwa masikini kutokana na kuwatumikisha  wananchi kuilisha nchi na  matajiri, huku wakiwa wanakabiliwa na changamoto kubwa.

Kutokana na hali hiyo, imesema sera imepitwa na wakati ambapo wizara  imelazimika kuanza kuipitia upya  na kuondoa  changamoto  na vikwazo kwa wakulima.

Bashe ametoa kauli hiyo  Jumamosi Agosti 3, 2019 wakati akifungua maonesho ya Nanenane  Mikoa ya Kagera,  Geita na Mwanza yaliyofanyika viwanja vya Nyamhongoro jijini Mwanza ambapo aliwapiga marufuku wakuu wa wilaya na mikoa kuwazuia wakulima kuuza chakula chao kwa kuhofia uwepo wa njaa.

Alisema kila mkulima, anajua namna anavyotunza  na kuilisha familia yake hivyo  kama kuna kiongozi anahofia uwepo wa njaa ni vema  akanunua mazao hayo  kwa bei anayotaka mkulima na kuyatunza ili yaweze kusubiria dhana aliyoiweka kichwani kwake, kwamba kutakuwapo na uhaba wa chakula.


"Nataka niwaulize hata kama tumejaza mahindi hiki kiwanja chote kama hamna hela ya kuyanunua hayo mahindi yatawasaidia? Wakulima wanalima mazao ya kilimo, ya chakula na ya biashara ili kupata uwezo wa mifuko yao.”

"Hatuwezi kujenga viwanda wakati wakulima ni masikini, haiwezekani na ili wakulima waweze kupata fedha ni lazima tuwaruhusu kufanya biashara za mazao yao pale ambapo wanaweza kuuza mazao yao,” alisema Bashe

“Sera iliyopo imepitwa na wakati  kabisa,  inawaumiza wakulima   na kuwafanya kubaki  kila mwaka kuilisha nchi na matajiri huku wao wakibaki na umasikini wao  huku kukiwapo na utitiri wa taasisi nyingi ambazo ukichunguza zimeanzishwa kwa lengo la kuwakandamiza, hii haiwezekani kama wizara tumeanza kuangalia ni taasisi gani zinatakiwa  kufutwa na kubaki  chache.

“Fedha ambazo zilikuwa zikielekezwa kwenye utitiri wa taasisi hizo, zitaelekezwa katika mfuko maalum  ambo  wizara tunatarajia kuanzisha  na kazi ya mfuko huo ni kufidia mkulima pale inapotokea mtikisiko wa bei katika soko la dunia, kama serikali hatuna uwezo wa kuthibiti bei ya soko la dunia, mfuko huo ndio utakaokuwa na kazi ya kutafuta fedha kwa ajili ya kuwafikia wakulima,”alisema.

Alisema Serikali ilikuwa ikipokea fedha nyingi kutoka mataifa ya nje ili kuendeleza kilimo, lakini zilikuwa zikishia katika semina mafunzo kwa  watendaji, huku  asilimia 50 ya fedha zilizokuwa zikipokelewa ndizo  zinafika kwa wakulima.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527