BALOZI SEIF AWAHAKIKISHIA WAKULIMA WA PAMBA KISHAPU KUWA YOTE KUNUNULIWA

Wakulima wa zao la Pamba wilayani Kishapu mkoani Shinyanga wamehimizwa kuendelea kulima zao hilo kwa wingi kwani serikali inaendelea kusimamia na kuhakikisha Pamba yao inanunuliwa kwa bei nzuri na kuwanufaisha zaidi.

Hayo yamesemwa jana  na Makamu wa pili wa Rais Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alipokuwa akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kata ya Somagedi na kuwahakikishia kuwa serikali imeshaweka sawa mipango yote na pamba yote itanunuliwa.

Awali akitoa taarifa ya utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM Mbunge wa Kishapu Mhe. Suleiman Nchambi amesema kuwa wakulima wa Pamba msimu huu wamepata shida kuuza Pamba yao kutokana na wanunuzi kutokwenda kununua Vijijini hali iliyowalazimu wakulima kuuza kwa bei ya hasara na Mbunge huyo kuiomba serikali kuwasaidi wakulima hasa suala la bei.

Akizungumza katika mkutano huo, Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Nyabaganga Talaba amesema kuwa serikali imeshaongea na mabenki na tayari yameshatoa fedha kwa wanunuzi na Pamba imeshaanza kununuliwa kwa bei iliyopangwa hivyo wakulima wasiwe na wasi wasi.

Katika hatua nyingine Mbunge Nchambi ametoa mifuko 1,200 ya saruji na mabati 400 kwaajili ya kumalizia ujenzi wa miradi mbalimbali ikiwemo shule, Zahanati na Vituo vya Afya, iliyoanzishwa na wananchi katika Kata zote 25 za Wilaya ya Kishapu.

Na Annastazia Paul - Malunde 1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527