MTOTO WA DEREVA WA MKUU WA MKOA WA MARA ALIYEPATA AJALI AKIENDESHA GARI LA RC AFARIKI DUNIA


Mtoto wa Dereva wa Mkuu wa Mkoa wa Mara Kasobi Shida mwenye umri wa miaka 26, aliyekuwa amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Musoma baada ya kupata ajali wakati akiendesha gari ya Mkuu wa Mkoa,Adam Malima amefariki dunia usiku wa kuamkia leo.



Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara Juma Ndaki amethibitisha kutokea kwa kifo hicho ambapo amesema,  kifo hicho kimetokea kwa sababu ajali aliyoipata ilikuwa ni mbaya hali iliyopelekea kijana huyo kupata majeraha ndani ya mwili wake.


''Ni kweli amefariki na sababu ya kifo chake, baada ya madaktari kumfanyia upasuaji waligundua utumbo wake umepasuka na damu imevujia ndani kwa ndani'' amesema RPC Ndaki.

Aidha Kamanda Ndaki akielezea hali ya Dereva wa Mkuu wa Mkoa (Baba wa Marehemu), amesema hali yake inaendelea vizuri na kwamba madaktari wanaendelea kumfanyia ushauri wa kisaikolojia ili arejee kwenye hali yake ya kawaida.

Kasobi Shida alipata ajali siku ya Agosti 4, baada ya kuchukua gari hilo bila ridhaa ya mzazi wake ambapo lilimshinda kuendesha na kutoka nje ya barabara kisha  kugonga daraja.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527