MO DEWJI AMMWAGIA SIFA RAIS MAGUFULI


Mkurugenzi wa Kampuni za Mohamed Enterprises Limited, Mohamed Dewji amempongeza Rais Magufuli kwa mageuzi makubwa kwa kipindi kifupi  cha uongozi wake.

Dewji ameyasema hayo leo akifungua kiwanda cha kusaga unga wa mahindi na ngano cha 21st Century Food Packaging kinachomilikiwa na Kampuni za Mohamed Enterprises Limited chenye uwezo wa kusaga tani 1,540 kwa siku

“Mheshimiwa Rais tunaamini kwamba wale wasiokuelewa leo watakuelewa baadae na wasioelewa lengo wataeleweshwa na matokeo ambayo tunaamini hayako mbali sana kwani mageuzi makubwa chini ya uongozi wako ndiyo yaliyotushawishi kuendelea kuwekeza nchini kama unavyoshuhudia leo hii,” amesema.

“Binafsi ninashuhudia kuimarika nidhamu kwa watumishi wa umma, mkazo mkubwa serikalini, kutekelezwa kwa miradi mbalimbali ya maendeleo, kupungua kwa rushwa na kushughulikiwa kwa migogoro ya ardhi nchini pia tumeguswa na namna ulivyoshugulikia matatizo ya wafanyabishara,” amesema.

Aidha amesema kiwanda hicho ni miongoni mwa viwanda vikubwa na vya kisasa kinachojihusisha na uzalishaji wa unga wa ngano na wa mahindi nchini, na kwamba kampuni ilianza uwekezaji 2005 na ilianza na kiwanda chenye uwezo mdogo wa kusaga tani 240 kwa siku pamoja na uwezo wa kuhifadhi tani 20 tu za nafaka.

“Hivi sasa kiwanda kimeboreshwa kwa kuwekeza kwenye mitambo mikubwa iliyogharimu jumla ya Sh. bilioni 105 na inatumia teknolojia ya kisasa zaidi, uwekezaji huu umefanyika chini ya awamu ya tano, leo tunashuhudia kiwanda cha mahindi chenye uwezo wa kusaga tani 300 kwa siku, kiwanda cha ngano chenye uwezo wa kusaga tani 1240 kwa siku, mitambo yenye uwezo wa kupokea tani 600 kwa saa za nafaka na uwezo wa kuhifadhi nafaka hadi tani elfu 50,” amesema.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527