LUKUVI AMREJESHEA ENEO LAKE BRIGEDIA JENERALI MSTAAFU BAADA YA KULIHANGAIKIA KWA MIAKA 20


Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi amemrejeshea eneo lake lililoko Jangwani Beach wilaya ya Kinondoni Dar es Salaam Brigedia Jenerali Mstaafu Francis Mbena kufuatia kuhangaika kwa miaka 20 kulirejesha eneo alilodhulumiwa.

Akizungumza wakati akimkabidhi hati ya kiwanja chake leo eno la Mbezi Beach Dar es Salaam Lukuvi alisema,  Brigedia Mstaafu Mbena alitaka kudhulumiwa eneo lake na Idan Mongi aliyeuziwa eneo hilo na  John Rwechungura.

Kwa mujibu wa Lukuvi,  kiwanja hicho chenye ukubwa wa takriban mita za mraba 2000 hati yake iligushiwa na baadaye kiwanja hicho kuuzwa kwa Mongi ambapo alieleza mnunuzi huyo alitapeliwa kwa kuwa kiwanja kilikuwa kimefutwa.

Lukuvi alitoa onyo kwa wanasheria kuacha tabia ya kuchelewesha kesi kwa kutowaeleza ukweli wateja wao iwapo kesi wanayoishughulikia hawezi kushinda na kufafanua kuwa ni bora wanasheria wakawaeleza ukweli kuhusiana na mwenendo wa kesi wanazoziendesha kuhusina na masuala ya ardhi.

Aidha,  amewataka wananchi wanaotaka kununua viwanja kufanya utafiti katika ofisi ya Msajili wa Hati Wizarani kwa lengo la kujiridhisha umiliki wa muuzaji wa eneo husika.

Kwa upande wake Brigedia Jenerali Mstaafu Mbena amefurahishwa na uamuzi uliofanywa na Lukuvi wa kumpatia hati yake  aliyoihangaikia kwa miaka 20 na kueleza kuwa eneo hilo limekuwa likimtesa sana kwa kuendesha kesi kwa muda mrefu na kutumia fedha yake ya pensheni kuendeshea kesi.

Mbena alisema eneo hilo alilipata mwaka 1988 Oktoba 3 na kuingia katika mgogoro baina yake na watu wanaodai kulimiki kuanzia mwaka 1999ambapo kesi ilianzia Baraza la Ardhi na Nyumba na kufikia Mahakama Kuu amapo  iliisha mwaka jana Julai na Mbena kushinda.

Naye Idan Mongi aliyetapeliwa kiwanja hicho alieleza kuwa kiwanja alichotapeliwa  kina historia ndefu ambapo kabla yeye kukinunua kilipitia kwa wamiliki wengine watatu na kubainisha kuwa yeye alikinunua kwa John Rwechungura mwaka 2009.

Alisema kuwa,  anamkabidhi eneo lake Brigedia Mstaafu Mbena kwa moyo mmoja na hatabomoa nyumba na ukuta aliojenga  na ameomba kuhamisha vitu vyake ndani ya miezi mitatu.

Lukuvi alisema, kutokana na uungwana aliounesha Idan Mongi Wizara itamzawadia kiwanja katika eneo la Pemba na Mnazi Kigamboni kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya kuishi tu.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527