ASKOFU ATAKA RAIS MAGUFULI AENDELEE KUUNGWA MKONO

Na Dotto Mwaibale, Singida


ASKOFU mstaafu wa Kanisa la Pentekoste (FPCT) la Singida Kati, Dkt.Paul Samwel (pichani) amewahimiza Watanzania kuunga jitihada zinazofanywa na Rais Dkt.John Magufuli za kuiletea nchi maendeleo.


Aliyasema hayo hivi karibuni katika hafla ya makabidhiano ya kituo cha kupima uoni na usikivu kwa wanafunzi wa shule za sekondari na msingi ziliopo mkoani hapa ambapo kituo hicho kimewekwa Shule ya Msingi Mahembe kikisimamiwa na kanisa hilo chini ya mradi wa elimu jumuishi.



Askofu Samuel alisema ana uhakika kuwa kila mtanzania mwenye mapenzi mema na uzalendo ni lazima ataziunga mkono jitihada za Rais Dkt.John Magufuli za kutuletea maendeleo nchini.


"Rais Magufuli alipoingia madarakani alianza kwa kusema Tanzania sio nchi maskini lakini baadhi yetu hatukumuelewa lakini baada ya muda mfupi tuliona miradi mikubwa ya maendeleo ikianza kufanyika ikiwa ni pamoja na kununuliwa kwa ndege kubwa za kisasa

tena kwa fedha taslimu" alisema Dkt.Samwel.


Alisema pamoja na miradi hiyo kuendelea kujengwa hatujawahi kusikia malalamiko ya wakandarasi kukosa pesa za malipo baada ya kukamilika kwa miradi hiyo na kuwa sasa hivi ile tabia ya nchi kuwa ombaomba imebaki kuwa ni historia.


Mgeni rasmi wa hafla hiyo Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida, Omari Kissuda alilshukuru kanisa hilo kwa msaada huo na kueleza utasaidia ufaulu kwa wanafunzi hao.


Afisa Tawala wa mradi huo, Karistoni Mwenda alisema ukarabati wa kituo hicho kuanzia chumba cha upimaji na vifaa vyake na ujenzi wa ngazi mterezo umegharimu sh.milioni 7.6 ambapo aliiomba Manispaa ya Singida kusaidia kuweka kiyoyozi kwenye chumba cha upimaji.


Mwenda alisema mradi huo umefadhiliwa na Shirika la misaada la Denmark (DANIDA) kupitia shirka la misaada la Danish Mission Council Development (DMCDD) likishirikiana na International Aid Service (IAS).




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527