ALIYEJIFANYA ASKARI AMEPANDISHWA KIZIMBANI


Mkazi wa Tabata Segerea David Ramadhani (33) aliyejifanya Askari wa Jeshi la Wananchi amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni Dar es salaam kwa makosa mawili likiwemo kukutwa na vifaa vya Umma.

Akisomewa hati ya mashtaka mbele ya Hakimu Joyce Moshi na Mwendesha Mashtaka wa Serikali ASP Hamisi alidai julai 19, 2019 eneo la  Makao Makuu JKT Mlalakua wilayani Kinondoni Dar es salaam kwa nia ya udanganyifu alijitambulisha kuwa ni Askari wa Jeshi la Wananchi kwa cheo cha MP.

Katika shtaka la pili julai 19, 2019 eneo la Makao Makuu ya JKT Mlalakua wilayani Kinondoni Dar es salaam alikutwa na vifaa vya Umma kinyume na sheria kama sare kamili za askari, sare za askari za kijani, beji na vyombo vya askari, kofia ya askari, kofia ya askari wa usalama wa barabarani, sare za viatu za askari , buti, pingu na redio call.

Mshtakiwa alikana kutenda shtaka mbele ya Mahakama na ASP Hamisi alisema upelelezi wa shauri hili unaendelea tunaomba tarehe nyingine ya kutajwa.

Hakimu Moshi alisema dhamana yake ipo wazi kwa masharti ya kuwa na wadhamini wawili waaminifu wenye kusaini bondi ya sh 2,000,000 kila mmoja, barua za utambulisho na nakala ya vitambulisho.

Mshtakiwa alishindwa kutimiza masharti ya dhamana na kurudishwa rumande hadi kesi yake itakapo kuja kusomwa tena septemba 2 mwaka huu.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527