WANAUME WANAONYONYA MAZIWA YA WANAWAKE WAONYWA


Francis Godwin-Mtanzania Iringa
WANAUME wenye tabia ya kunyonya maziwa ya wanawake pindi wanapokuwa kwenye jukumu la kunyonyesha watoto wao, wametakiwa kuacha kwani kufanya hivyo ni kosa kisheria.

Imeelezwa kuwa kufanya hivyo ni ukatili wa kijinsia ambao hufanyiwa wanawake na watoto katika ngazi ya familia.

Hayo yalisemwa jana mjini hapa na Ofisa Lishe wa Mkoa wa Iringa, Neema Mtekwa, alipokuwa akijibu maswali kwa waandishi wa habari katika warsha ya siku moja, ikiwa ni maandalizi ya Wiki ya Unyonyeshaji Duniani.

Neema alisema wanaume wenye tabia za kunyonya maziwa ya wake zao wakati wakiwa wananyonyesha hawatendi haki kwa mtoto kwani yeye hutegemea maziwa kama chakula chake wakati wote.

Alisema kwa mujibu wa utaratibu, mama anapojifungua hutakiwa kunyonyesha mtoto kwa muda wa miezi sita bila kumpa chakula chochote, lakini wakati mwingine wapo kina baba hunyonya maziwa ya mama huku mtoto akikosa lishe yake sawasawa.

“Kimsingi mama anatakiwa kuanza kumnyonyesha mtoto wake mara baada ya kujifungua ndani ya saa moja ili kusaidia maziwa kutoka mapema. 

“Maziwa ya mama ni kwa ajili ya mtoto ila kuna tabia ambayo inasemwa na bado haujafanyika utafiti wa kina, kwamba wapo baadhi ya wanaume wanapenda kunyonya maziwa wake zao wakijifungua, ambayo ni maalumu kwa ajili ya mtoto, huu ni ukatili mkubwa dhidi ya mtoto,” alisema Neema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527