RAIS MAGUFULI AITAKA WIZARA YA MALIASILI IWEKE MIKAKATI KUONGEZA WATALII


Rais Magufuli ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kuweka mikakati madhubuti ya kuongeza watalii nchini ambao ametaja baadhi ya malalamiko ambayo amekuwa akiyapata kupitia ripoti ya robo mwaka na kiitaka wizara hiyo kuhakikisha inafanya kazi masuala hayo.

Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo Jumanne Julai 9, wilayani Chato mkoani Geita katika uzinduzi wa Hifadhi ya Taifa ya Burigi – Chato yenye ukubwa wa kilometa za mraba 4,702.

“Ninatoa wito kwa Wizara ya Maliasili na Utalii kuendelea kujipanga na kuweka mikakati madhubuti ya kuongeza watalii nchini, miongozi mwa malalamiko ambayo nimekuwa nikiyapata ni pamoja na gharama za utalii kuwa juu, usafi kwenye hoteli na mengine mengi hivyo hamna budi kufuatilia mambo hayo,” amesema.

“Ninawasihi kuwa na utaratibu wa kufanya kaguzi mara kwa mara lakini pia wekeni mikakati ya kujenga uwezo wa waongoza watalii na kuhakikisha wote wanatambuliwa rasmi maana kuna wengine wanadanganya watalii, hakikisheni hifadhi zetu zinakuwa na mchanganyiko mzuri wa vivutio,” amesema.

Aidha amewataka watanzania kujega utamaduni wa kutembelea vivutio vya ndani hasa katika maeneo ya hifadhi zinazowazunguka ili kuiongezea nchi kipato na kukuza uchumi wa nchi ambapo ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kuweka gharama nafuu kwa watalii wa ndani ili kuwezesha zoezi hilo.

“Ninahimiza Wizara kuendelea kuhamasisha utalii wa ndani ikiwemo kwa kuweka gharama za nafuu pia kwa watanzania ninawasihi kujenga utamaduni wa kutembelea vituo vyetu vya utalii pia tuanzisha hifadhi ndogo ndogo za kufuga wanyama pori,” amesema.

“Mimi ninafikiria kuanzisha hifadhi ndogo lakini nitafuga wale wanyama ambao ni wapole nisije nikajikuta nimekuwa kitoweo huko ndani, ninasisitiza Wizara hakikisheni mnaangalia gharama kwa wazawa zinakuwa chache,” amesema.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527