MAMIA YA WAANDAMANAJI WAKAMATWA URUSI


Polisi mjini Moscow Urusi wamewakamata takriban watu 1000 waliokuwa wakiandamana kushinikiza uchaguzi wa mitaa ufanyike kwa njia ya uhuru na haki.

Takriban watu 3,500 walishiriki kwenye maandamano hayo ambayo hayakuruhusiwa na maafisa wa serikali.

Waandishi wa habari wa shirika la AFP waliokuwepo eneo hilo wamesema polisi walitumia vigongo na mabomu ya kutoa machozi dhidi ya waandamanaji.

Maandamano ya jana yalijiri, wiki moja tu baada ya maandamano makubwa kufanyika mjini Moscow ambapo waandamanaji 22,000 waliwataka maafisa kubadilisha uamuzi na wawaruhusu wanaharakati wa upinzani kugombea viti kwenye uchaguzi wa mji utakaofanyika mwezi Septemba.

Tangu uamuzi huo ulipotolewa, wachunguzi wamekuwa wakifanya msako majumbani na katika makao makuu ya wagombea waliokataliwa, huku mkosoaji mkubwa wa serikali Alexei Navalny akifungwa jela kwa siku 30 kwa kuitisha maandamano mapya.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527