AJALI YA HIACE,LAND CRUISER YAUA SITA NA KUJERUHI 12 KAHAMA


Gari aina ya Toyota Hiace yenye namba za usajili T 710 AZZ iliyopata ajali.
Gari aina ya Land cruiser yenye namba za usajili T 477 ATC lililopata ajali. 

Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Richard Abwao 


Na Salvatory Ntandu- Malunde1 blog Kahama

Watu sita wamefariki dunia na wengine 12 kujeruhiwa baada ya gari aina ya Toyota Hiace yenye namba za usajili T 710 AZZ na kugongana uso kwa uso gari aina ya Land cruiser yenye namba za usajili T 477 ATC katika eneo la Nyambura kata ya Ngogwa Mjini Kahama mkoani Shinyanga 



Ajali hiyo imetokea jana Jumapili Julai 21,majira ya saa moja na nusu usiku.


Kwa mujibu wa Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Richard Abwao amesema gari aina ya Land Cruiser iliyokuwa inaendeshwa na Thomas Evarist Katoto (47) likitokea Kahama Mjini kwenda Kakola liligongana uso kwa uso na gari aina ya Hiace likiendeshwa na dereva aliyejulikana kwa jina moja la Enock (32) mkazi wa Kakola likitokea Kakola kwenda  Kahama Mjini.

"Ajali hiyo ilisababisha vifo vya watu wanne waliokuwa kwenye Hiace ambao ni  Buruani Yassin Haule (32) mkazi wa Kakola na watoto watatu wakiwemo wawili wa kike wanaokadiriwa kuwa na miaka mitatu hadi mitano,na kujeruhi watu 12 na sasa idadi ya vifo imeongezeka kutoka vinne hadi sita" ,amesema Kamanda Abwao.

Amesema chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi wa magari yote mawili na miili ya marehemu imehifadhiwa katika hospitali ya halmashauri ya Mji wa Kahama.

Aidha ameeleza kuwa barabara ya Kakola - Kahama imekuwa na vumbi nyingi kutokana na kutumika na magari mengi baada ya kuibuka kwa machimbo mapya ya Kakola Namba 9 na kuwataka madereva wote kuchukua tahadhari kwa kutoendesha kwa mwendo kasi ili kuzuia ajali.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527