WAZIRI MWAKYEMBE AZINDUA KAMPENI YA KUICHANGIA TIMU YA TAIFA “TAIFA STARS”


Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe amezindua rasmi kampeni maalumu ya kuchangia timu ya Taifa “Taifa Stars” inayoshiriki mashindano ya Kombe la Maifa ya Afrika (AFCON) yanayotarajiwa kuanza Juni 21 nchini Misri.


Waziri Mwakyembe amesema watanzania hawana budi kuchangia kiwango chochote na kwamba fedha hiyo itakuwa salama na itawafikia wachezaji hao bila ya mizengwe yoyote.

"Watanzania kote nchini wanaweza kuichangia timu yao  kupitia akaunti zifuatazo BMT N BC 011101000978, Sport Development Fund, CRDB 01J1019956700 na Voda *150*00#5595298. Ukichangia, ujumbe unaopata utume  kwenda 0735 414043 jina litakuja Oscar Zabloni ambye ni mweka hazina ,'' amesema Dkt. Mwakyembe.

Amesema wote watakaochangia watapewa cheti  maalumu na  kiongozi wa kitaifa ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wao katika kuhakikisha timu yetu ya Taifa inafanya vizuri katika mashindano hayo.

Naye mwenyekiti wa kamati ya kusaidia Taifa Stars, Paul Makonda amesema siku ya Jumamosi Juni 22, 2019 mkoa wa Dar es Salaam utafanya maombi maalum kwa ajili ya  kuiombea timu ya Taifa Stars ambayo inatarajia kushuka dimbani siku ya Jumapili Juni 22 dhidi ya timu ya Taifa ya Senegal.


Pamoja na mambo mengine Makonda amezitaka kampuni 41 zilizoahidi kuchangia Taifa Stars kutoa michango hiyo.

"Jumamosi ya Juni 22,2019 Mkoa wa Dar es Salaam tutafanya maombi maalum kuiombea timu ya Taifa Stars, na pia nitumie nafasi hii  kuyakumbusha  makampuni  yaliyoahidi kuichangia Taifa Stars sasa wachangie kupitia akaunti hizo,'' amesema Makonda.


Timu ya Taifa Stars iko kundi C, pamoja na timu za Senegal, Algeria na Kenya ambapo siku ya Jumapili inatarajia kutupa karata yake ya kwanza dhidi Senegal.

Tayari Stars imeshacheza mechi mbili za kirafiki za kujipima nguvu, huku ikipoteza mchezo wake wa kwanza dhidi ya Misri 1-0 na kutoka sare ya goli 1-1 dhidi ya Zimbabwe.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527