KIPA BENNO KAKOLANYA ATUA RASMI SIMBA

Hatimaye kipa Benno Kakolanya amesaini rasmi mkataba wa miaka miwili kuitumikia Simba kuanzia msimu ujao.

Kakolanya ambaye sehemu ya msimu uliopita aliitumikia Yanga kabla ya kuafikiana na klabu yake hiyo ya zamani kuvunja mkataba sasa atakuwa mali ya Simba.

Mgogoro wa Kakolanya na Yanga ulitokana na madai ya malipo ya fedha kabla kipa huyo kujiondoa katika kikosi hicho ambapo kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera aliamua kumtimua na kugoma kumrejesha.

Kakolanya sasa amesaini mkataba huo na Simba akiwa mchezaji huru huku Simba wakinufaika na vita ya kipa huyo na Zahera.

Usajili huo una maana kwamba sasa Kakolanya anakwenda kupigania namba na kipa namba moja wa Simba na timu ya taifa, Aishi Manula.

Wawili hao ndiyo waliokuwa makipa wa Stars wakati Kakolanya akiwa na Yanga ambapo sasa kama Simba kupitia benchi lake la ufundi litaendelea kuwa na maamuzi ya kumtumia kipa mmoja namba moja katika mechi nyingi huenda wawili hao mmoja akapoteza nafasi ya kuwa timu ya taifa.

Hata hivyo kwa hali inavyoendelea kupitia usajili huo ni wazi kipa Deogratias Munishi 'Dida' akakimbia timu hiyo kutokana na Manula tayari amesaini mkataba wa kuendelea kuiongoza timu hiyo.

Hatua ya Dida kuondoka itatokana na kipa huyo kukosa uhakika wa kupata nafasi kufuatia msimu uliopita kupata mechi chache ingawa pia alifanya vizuri katika mechi alizocheza.

Dida amemaliza mkataba wake na Simba na habari za ndani zinasema mabosi hao hawana mpango wa kumwongeza mkataba.
Na Khatimu Naheka - Mwanaspoti

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527