RAIS MSTAAFU AJIUNGA NA CHAMA CHA UPINZANI


Rais mstaafu wa Botswana, Ian Khama amejiengua katika chama tawala kilichoongoza nchi hiyo tangu uhuru miaka 53 iliyopita, akieleza tofauti kubwa baina yake na Rais aliyerithi kiti chake.

Hii ni mara ya kwanza kwa Botswana kuona rais mstaafu anakitosa chama cha tawala cha Botswana Democratic Party (BDP).

Khama mwenye umri wa miaka 57, alisema hakuwa na chama chochote lakini ataunga mkono chama cha upinzani cha Umbrella for Democratic Change (UDC) kupambana na BDP.

Khama aliyeingia madarakani Aprili Mosi 2008 akimrithi Festus Mogae, aliwaeleza maelfu ya wafuasi wake katika mji wa nyumbani kwake wa Serowe jana kwamba alifanya makosa katika kumteua Mokgweetsi Masisi kuwa rais.

Nimekuja hapa leo kuwaeleza kwamba ninaachana na BDP. Ninaitupa kadi yangu ya uanachama wa BDP,” alisema Khama huku akitupa kadi yake. “Siitambui BDP tena,” aliongeza.

Maelfu ya watu waliofurika katika mkutano huo, pia walirusha kadi zao za BDP.

Khama na mrithi wake wamekuwa wakilumbana waziwazi kutokana na Masisi kubadili sera zilizoanzishwa na mtangulizi wake, ikiwamo ya hivi karibuni ya kuondoa zuio la uwindaji wa tembo.

Tangazo la kuondoa zuio hilo lilitolewa Machi mwaka huu na Khama alimshutumu ‘kijana wake’ kwa usaliti.

Botswana ina ukomo wa vipindi viwili vya urais. Masisi alichukua madaraka baada ya Khama kujiuzulu Machi mwaka jana.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527