SERIKALI YAENDELEA KUWA NA DHAMIRA YA KUONDOA KERO KWA WACHIMBAJI WADOGO WA MADINI


Na.Faustine Gimu Galafoni,Dodoma.
Serikali imedhamiria kuondoa kero  kwa wachimbaji wadogo  wa Madini hapa nchini  ikiwa ni pamoja na kero za kuondolewa na wachimbaji wakubwa   kwani  asilimia kubwa wachimbaji wadogo  ndio wagunduzi wa kwanza kwenye maeneo ya  Madini. 


Hayo yamesemwa leo Mei 21,2019 bungeni jijini  Dodoma na Naibu waziri wa Madini Stanslaus Nyongo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum  Rhoda Kunchela aliyehoji serikali iko tayari kutatua kero za wachimbaji wadogo  na vibarua ambao wananyanyasika nchini. 


Katika Majibu yake  Naibu Waziri Stanslaus Nyongo amesema viongozi wanaonyanyasa wenzao serikali ipo tayari kuwafutia leseni zao huku akisema kuwa  serikali imekuwa ikiendelea kutatua migogoro ya Wachimbaji wakubwa na wadogo wanaovamia kwenye maeneo yasiyo ya kwao. 


Aidha ,Mhe.Nyongo amefafanua kuwa hata mchimba kokoto ana wajibu wa kulipia kitambulisho cha Wajasiliamali wadogo ambacho kilitolewa na Rais John Pombe Magufuli kwa ajili ya Maendeleo ya nchi. 


Waziri mwenye dhamana ya Madini, Mhe.Dotto Biteko  ametoa wito kwa watozaji wa kodi za madini zilizoondolewa Bungeni waache Mara moja  kwani imebainika kuna baadhi ya maeneo hapa nchini wanaendelea kutoza. 


Migodi yote nchini inaendeshwa kwa mujibu wa sheria ya madini ya mwaka 2010  na marekebisho yake ya mwaka 2017 na kuzingatia kanuni za uchimbaji,usalama,mazingira na Afya kwa wakazi.

 


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post