ILE ALMASI KUBWA KULIKO ZOTE YAUZWA BILIONI 3.2 SHINYANGA


Joseph Temba, mchimbaji mdogo wa madini mkoani Shinyanga leo Jumamosi Mei 25, 2019 ameuza jiwe la almasi kwa Sh3.2bilioni katika soko la madini la Mkoa wa Shinyanga.


Mauzo ya almasi hiyo yenye uzito wa Kareti 512.15 yamefanyika jana katika soko la madini Mkoa wa Shinyanga na kushuhudiwa na naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo na Kamishna wa Tume ya Madini, Profesa Abdulkarim Mruma.

Akizungumzia mauzo hayo, Nyongo amesema kutokana na mauzo hayo Serikali itapata Sh238milioni.

Amebainisha kuwa lengo la Serikali ni kuwezesha shughuli za wachimbaji wadogo na wadau wote wa sekta ya madini kufanyika kwa utaratibu unaoeleweka kwa faida yao na ya Serikali.

“Nimpongeze Joseph ameuza almasi yake hapa kila kitu kinakuwa wazi mbele ya Serikali, polisi, watu wa usalama na wawakilishi wa Benki ya CRDB tena bila usumbufu wowote na hiki ndicho tunachokitaka,” amesema Nyongo.

Kwa upande wake Temba ameishukuru wizara hiyo kwa utaratibu waliouweka katika kutoa mwongozo na usimamizi wa namna ya mauzo ya madini unavyotakiwa kufanyika.

“Natoa wito kwa wachimbaji wadogo hakuna sababu ya kuyakimbia masoko yaliyoanzishwa na Serikali yana faida nyingi ikiwemo usalama, ulinzi, uwazi na utambuzi wa thamani halisi ya madini kitu ambacho ni nadra sana kwenye masoko yasiyo rasmi,” amesema Temba.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527