SERIKALI: WAZABUNI WATIA KIBINDONI SHILINGI BILIONI 199


Serikali imeleeza kuwa imeshawalipa Wazabuni 2048 kiasi cha Shilingi 199 tangu kutolewa kwa tamko la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 3 Januari, 2018 Ikulu Jijini Dar es Salaam la kutaka Wazabuni wote wanaoidai Serikali walipwe.

Hayo yameelezwa Bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, alipokuwa akijibu swali la msingi la Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Iringa (CCM), Mhe. Ritta Kabati, aliyetaka kujua baada ya tamko la Mhe. Rais kuhusu Wazabuni wote wanaoidai Serikali walipwe ni Wazabuni wangapi wameshalipwa.

Akijibu swali hilo Dkt. Kijaji alieleza kuwa kati ya Wazabuni 2048 waliolipwa na Serikali, Wazabuni 1,277 walihudumia Sekretarieti za Mikoa na 771 walihudumia Wizara, Taasisi na Wakala za Serikali.

Dkt. Kijaji alifafanua kuwa Shilingi 3,729,605,175 zimetumika kulipa Wazabuni waliotoa huduma kwa Sektretarieti za Mikoa na Shilingi 195,334,409,791.64 zimetumika kulipa Wazabuni wa Wizara, Taasisi na Wakala za Serikali.

“Ikumbukwe kuwa madeni yote haya yalilipwa baada ya uhakiki kufanyika”, alisisitiza Dkt. Kijaji.

Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kulipa madai mbalibmali ya wazabuni kulingana na upatikanaji wa fedha, sambamba na uhakika wa madai husika.

Dkt. Kijaji amesema kuwa ili kukamilisha zoezi la uhakiki kwa wakati, wazabuni wote wanatakiwa kutoa ushirkiano, hususan kuwasilisha taarifa na vielelezo sahihi vya madai yao pindi wanapotakiwa kufanya hivyo.

Katika swali la nyongeza Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Kabati alitaka kujua vigezo vilivyotumika kuwalipa wazabuni hao.

Akijibu swali hilo la nyongeza Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji alisema kuwa vipo vigezo vingi ambavyo Serikali imevitumia kulipa madeni hayo moja ikiwa umri wa deni, madeni ambayo yamekaa kwa muda mrefu na ambayo tayari yamehakikiwa ndiyo yanapewa kipaumbele katika malipo.

Aliongeza kuwa kigezo cha pili ni riba Serikali imekuwa ikitoa kipaumbele kwa madeni ambayo riba yake inakuwa kulingana na muda, ili Serikali isiendelee kuumia wala mwananchi asiendelee kuumia.

Na Farida Ramadhani na Josephine Majura, WFM, Dodoma

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527