TFDA YATOA MSAADA WA TAULO ZA KIKE KWA WANAFUNZI 538 WALIO KAMBI ZA KITAALUMA SIMIYU

Mamlaka ya Chakula na Dawa(TFDA) imetoa msaada wa katoni 111 za taulo za kike zenye thamani ya shilingi milioni tano, kwa wanafunzi wa kike 538 walio katika kambi ya kitaaluma ya wanafunzi wa kidato cha sita mwaka 2019, inayoendelea katika Shule ya Sekondari ya wasichana Maswa Mkoani Simiyu.

Akikabidhi msaada huo Aprili 05, 2019 Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) Kanda ya Ziwa, Bi. Nuru Mwasulama, amesema Mamlaka hiyo imetoa msaada huo kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuinua elimu mkoani Simiyu, ili kuwasaidia watoto wa kike wasome kwa uhuru na utulivu kambini hapo hususani wakati wa hedhi.

Amesema TFDA kama wadau wa mkoa wataendelea kushirikiana na Serikali mkoani Simiyu katika sekta ya elimu na masuala mengine ya Maendeleo, huku akiwasisitiza wanafunzi  walio kambini kusoma kwa bidii na kutumia vizuri muda walionao  ili waweze kufikia malengo yao.

Akipokea msaada huo, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka ameishukuru Mamlaka hiyo kwa msaada  uliotolewa  kwa wanafunzi wa kike, huku akiwasisitiza wanafunzi wote walio katika kambi ya kitaaluma kusoma kwa bidii.

Aidha, Mtaka amewashukuru wadau mbalimbali ambao wameendelea kutoa michango kwa ajili ya kufaninisha  kambi ya kitaaluma inayoendelea mkoani humo, huku akiahidi kuwa wadau wote waliochangia watatambuliwa na kupewa vyeti.

Katika hatua nyingine Mtaka ametoa ufafanuzi kwa wadau na wananchi kuhusu utaratibu wa kambi za kitaaluma mkoani Simiyu, kwamba kambi hizi hufanyika katika ngazi za shule na baadaye huundwa kambi moja ya mkoa kuwakutanisha wanafunzi kwa ajili ya kambi ya mkoa.

“Kambi za Kitaaluma kwenye mkoa zilianza muda mrefu lakini kama mkoa tumeweka utaratibu wa kuwa na kambi moja ya kimkoa inayounganisha shule zote za kidato cha sita; kambi za kidato cha nne nazo zinaendelea kwa hiyo tutakapofika mwezi wa saba tutaanza kuunganisha shule, kama tulivyofanya mwaka jana tuliunganisha shule 24 pale Simiyu Sekondari” alisema.

Nao wanafunzi wa kike wa Kidato cha Sita walio katika Kambi hiyo ya Kitaaluma wameishukuru Mamlaka ya Chakula na Dawa kwa msaada huo ambao wamesema utawasaidia sana kusoma kwa uhuru na kujiamini zaidi wakati wa hedhi.

“Tulikuwa tunakumbana na changamoto ya kutokuwa na amani na kushindwa kujiamini wakati wa hedhi kwa hiyo hata kusoma tulikuwa tunasoma lakini tunakuwa na wasiwasi, kupitia msaada huu ‘tutakuwa comfortable ‘ (tutakuwa na amani) kabisa tunaishukuru sana TFDA”,Mwanaidi Halfan.

“Huu msaada tuliopata utanisaidia kufikia ndoto zangu maana wasichana wengi wanapokosa taulo hizi za kike wanashindwa kusoma, wanakuwa na hofu wengine hata darasani hawaendi, lakini kwa kuwa wote tumepata msaada huu najua muda tutakao kuwa hapa tutakuwa huru kujisomea hatutaogopa tena maana zinatuhakikishia usalama tunapokuwa hedhi” ,alisema Hidaya Simba.

Jumla ya wanafunzi 1166 wa kidato cha Sita mwaka 2019 kutoka shule 12 mkoani Simiyu wako katika kambi ya kitaaluma kwa siku 28 katika shule ya sekondari Maswa, kwa ajili ya maandalizi ya Mtihani wa Taifa unaotarajia kufanyika mwezi Mei, 2019.
Baadhi ya wanafunzi wa kikewa kidato cha Sita mwaka 2019 mkoani Simiyu wakiwa  katika picha ya pamoja na Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) Kanda ya Ziwa, Bi. Nuru Mwasulama (katikati), mara baada ya kupokea msaada wa taulo za kike zilizotolewa kwa ajili yao na mamlaka hiyo, katika  kambi ya kitaaluma ya wanafunzi wa kidato cha sita mwaka 2019 inayoendelea katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Maswa mkoani Simiyu.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(wa pili kushoto)akiwa na baadhi ya wanafunzi wa kike wa kidato cha sita mkoani humo, wakipokea sehemu ya msaada wa taulo za kike zilizotolewa na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) na kuwasilishwa na Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) Kanda ya Ziwa, Bi. Nuru Mwasulama (wa tatu kulia), katika  kambi ya kitaaluma ya wanafunzi wa kidato cha sita mwaka 2019 inayoendelea katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Maswa mkoani Simiyu.
Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) Kanda ya Ziwa, Bi. Nuru Mwasulama (wa pili kulia) akimkabidhi Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(kushoto) na baadhi ya viongozi wa Mkoa wa Simiyu na baadhi ya wanafunzi  sehemu ya maboksi ya taulo za kike ambazo zimetolewa msaada kwa wanafunzi kike walio kwenye kambi ya kitaaluma ya wanafunzi wa kidato cha sita mwaka 2019 inayoendelea katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Maswa mkoani Simiyu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527