ASKARI MAGEREZA ANASWA NA PEMBE ZA NDOVU JIJINI DODOMA

Na.Faustine Gimu Galafoni,Dodoma

Jeshi La Polisi  Mkoa Wa Dodoma Linawashikilia Watu Watatu  Kwa Tuhuma Za Makosa Mbalimbali  Yakiwemo Kupatikana Na Nyara Za Serikali,kughushi Na Kujipatia Mali Kwa Njia Ya Udanganyifu.

Akizungumza na waandishi wa habari jana  April 3 ,kamanda wa polisi mkoa wa Dodoma  SACP.Gilles  Muroto alisema tukio la kwanza ni kupatikana na nyara za serikali  ambapo amebainisha mnamo tarehe 1 April, 2019  mtaa wa Kilimani wilaya na Jiji la Dodoma  alikamatwa  A.8070  SSGT Comas Joseph Ndasi  askari magereza wa gereza la Msalato [51] akiwa na pembe za ndovu  vipande 6 sawa na tembo 3  vye uzito wa kg 13 thamani ya Tsh.103,5000,000 alivyoficha kwenye mfuko  akiwa anamsubiri mteja kwa ajili ya kufanya mauzo.

Kamanda Muroto ametaja tukio la pili ni la Mohammed  Ahmed Hamis  ambaye amekamatwa kwa kosa la kujipatia  mali kwa njia ya udanganyifu  ambapo alijipatia magari mawili ,Toyota Land cruiser  V-8   Lenye namba za usajili T.366 BRX  rangi Nyeusi na gari No.T.581 DKS Toyota aina ya Noah .

Kamanda Muroto amefafanua tukio lilitokea Mikocheni  jijini Dar Es Salaam  mwaka 2017  ambapo mtuhumiwa alijitambulisha kwa mwenye magari  kuwa afisa  usalama  anahitaji magari kwa ajili ya kazi maalum  ambapo aliandika mkataba wa kukodi magari hayo  na alipoyapata alitoweka nayo  na hakurejesha  hadi alipokamatwa   April 2 jijini Dodoma .

Mtuhumiwa aliyatumia magari hayo pia kujipatia pesa kwa watu mbalimbali kwa kuyawekea dhamana  kukopa pesa  kisha kulitelekeza gari  na jeshi la polisi litampeleka  Dar es Salaam  alikoshitakiwa na atafikishwa mahakamani.

Na tukio la tatu ni la kujifanya Afisa wa serikali ambapo mnamo tarehe 26 Machi,2019 alikamatwa  Ambokile Hezron  Mwampulo [32]  akijifanya afisa usalama wa Taifa  akidanganya watu na kukusanya fedha  akiwaahidi kuwapatia ajira  katika idara ya usalama wa Taifa  na taasisi nyingine za serikali .

Kabla ya kukamatwa  alijipatia fedha kiasi cha Tsh.950,000 kutoka kwa watu wawili ambapo Tsh.550,000 kwa mtu mmoja na Tsh.400,000 kwa mtu wa pili.

Mtuhumiwa baada ya kukamatwa alifanyiwa upekuzi  Nyumbani kwake Ndachi jijini Dodoma  ambapo alikamatwa na nakala 15  za vyeti vya watu mbalimbali ,barua 3 za maombi ya ajira  za watu tofauti  na nakala ya leseni moja  na mtuhumiwa atafikishwa mahakamani.

Hata hivyo jeshi la polisi limetahadharisha watu kujihadhari  na matapeli  wanaotumia vibaya majina ya taasisi  za serikali na kuwaibia na serikali ina utaratibu wake wa kuajiri watu  .


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527