RAIS MAGUFULI ATOA ZAWADI YA VIWANJA KWA WACHEZAJI WOTE WA TAIFA STARS NA BONDIA MWAKINYO

Baada ya timu ya taifa ya Tanzania Taifa Stars kuifunga Uganda 3-0 katika mchezo wa kuwania kufuzu kucheza AFCON 2019 na kufuzu kwa mara ya kwanza baada ya miaka 39, Rais Magufuli aliwaita wachezaji Ikulu Dar es Salaam kwa ajili ya kuwapongeza na kuwapa zawadi wachezaji.


Kwanza; Rais Magufuli ametangaza kutoa Tsh Bilioni 1 kwa ajili ya maandalizi ya timu ya Taifa ya Vijana ya Serengeti Boys chini ya miaka 17 zinazofanyika Tanzania mapema mwezi April..

"Sikuwa na fedha kwa ajili ya kusaidia maandalizi, nimepigiwa simu na Waziri Mkuu, Makamu wa Rais lakini sikuwa nimesema chochote lakini kwa furaha tuliyonayo nitatoa kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya maandalizi ya timu yetu,”amesema Rais Magufuli.


Pili; Rais Magufuli ametoa zawadi ya viwanja kwa wachezaji wote wa Taifa Stars na kuwaagiza wapatiwe viwanja hivyo makao makuu ya nchi Dodoma, mchezaji wa zamani wa Taifa Stars Peter Tino aliyefunga goli la Taifa Stars kucheza AFCON 1980, Rais Magufuli amempa Tsh Milioni 5 baada ya mchezaji huyo kusema kuwa hana cha kufanya kwa sasa.


“Kila mmoja apate kiwanja chake, kama Serikali ilitoa viwanja kwa mabalozi wa nchi nyingine, hatuoni sababu ya mabaloz wa Taifa letu (Taifa Stars na Hassan)kwanini wasipatiwe viwanja. Haiwezekanani baada ya kustaafu wanabaki hawana kitu , lazima tutambue kazi ambayo wameifanya kwa niaba ya nchi yetu ,”amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli amesema anatambua mchezaji wa kimataifa na Nahodha wa Taifa Stars Mbwana Samatta ameondoka nchini jana kurudi kwenye timu yake lakini naye asisahaulike kwenye zawadi ya kiwanja huku akitumia nafasi kutoa maagizo kwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kusimamia upatikanaji wa viwanja hivyo.

Kuhusu mchezo wa jana amesema amefurahishwa na uchezaji wa Taifa Stars kwani wamejituma sana uwanjani na ukweli ni kwamba walikuwa wanapiga pasi nzuri .

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527