Tanzia : MAKAMU MWENYEKITI WA KLABU YA WAANDISHI WA HABARI ARUSHA CHARLES OLE NGEREZA AFARIKI DUNIA


Marehemu Charles Ole Ngereza enzi za uhai wake
Mwenyekiti wa Arusha Press Club (APC) Claude Gwandu akiwa msibani nyumbani kwa marehemu Charles Ngereza na baadhi ya waandishi kama wanavyoonekana pichani. 
Waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali Mkoani Arusha wakiwa msibani nyumbani kwa Marehemu Charles Ngereza eneo linalofahamika kama Kwa Mrefu.

Na Vero Ignatus, Arusha.


Makamu mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari mkoa wa Arusha (Arusha Press Club -APC) ambaye awali alikuwa Mwakilishi wa habari wa ITV na Radio One baadaye Idhaa ya Kiswahili DW mkoani Arusha Charles Ole Ngereza amefariki dunia leo Jumamosi Machi23,2019.

Marehemu alianza kuugua mwishoni mwa Mwezi Desemba 2018  ambapo alianza kupatiwa  matibabu katika  hospitali ya KCMC, ambapo alihamishiwa nchini India kwa matibabu zaidi na baadae alirudi nyumbani na kuendelea kujiuguza.

Hata hivyo hali yake ilibadilika ghafla hapo jana mchana na kukimbizwa katika hospitali ya Mkoa ya Mount Meru kisha kuhamishiwa Hospitali ya St. Elizabeth Mkaoni Arusha na kufariki dunia leo alfajiri.

Mwenyekiti wa Arusha Press Club Claude Gwandu amesema msiba huo ni mzito kwa wanahabari wa mkoa wa Arusha kwani marehemu alikuwa ni mchapakazi, asiyekuwa mvivu na alikuwa mtu wa viwango na ubora.

"Kama kiongozi mwenzetu tumeshirikiana nae katika mambo mengi sana hata hivi  alipoondoka kuna mradi alituunganisha na wadau wake katika klabu yetu wa zaidi ya milioni 500 ambao utaleta manufaa kwa wanachama wa APC na tunaamini kwamba wadau hao hawatausitisha",ameeleza Gwandu.

"Waandishi wa habari kwa pamoja Jijini Arusha wamesikitika kuondokewa mwenzao hivyo  ametoa pole kwa wanahabari na wote walioguswa na msiba huu",alisema Gwandu.

Kwa mujibu wa Gwandu mazishi yanatarajiwa kufanyika Jumatano wiki ijayo.

Marehemu ameacha mke mmoja na watoto wawili mmoja wa kike na mwingine wa kiume.

Bwana alitoa na Bwana ametwaa Jina lake Lihimidiwe.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527