MKURUGENZI JAMII FORUMS NA MWENZAKE WAKUTWA NA KESI YA KUJIBU

Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jamii Forums, Maxence Melo na mwenzake Mike Mushi, wamekutwa na kesi ya kujibu katika kesi ya kuzuia jeshi la polisi kufanya uchunguzi, inayowakabili viongozi wa mtandao huo.

Washitakiwa hao wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Ijumaa Februari 22, wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kutolewa uamuzi kama wana kesi ya kujibu au la, baada ya upande wa jamhuri kufunga ushahidi wa mashahidi watatu.

Akisoma uamuzi huo, Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba amesema baada ya kupitia ushahidi na kielelezo ambacho kilitolewa mahakamani hapo amejiridhisha pasi na shaka kuwa washtakiwa hao wana kesi ya kujibu.

Amesema washtakiwa hao wanaweza kujitetea kwa kula kiapo, bila kiapo au kukaa kimya na kusubiri uamuzi wa mahakama.

Baada ya kueleza hayo, wakili anayewatetea washtakiwa hao, Nashon Mkungu amedai kuwa wateja wake watajitetea kwa kiapo na wanatarajia kuwa na mashahidi watano.

"Upande wa utetezi tunatarajia kuleta mashahidi watano, hivyo tunaomba tarehe ya kuanza kujitetea" amedai wakili Mkungu.

Wakili wa utetezi baada ya kueleza hayo, Hakimu Simba amepanga Machi 14 na 19, 2019 washtakiwa hao waanze kujitetea.

"Washtakiwa wataanza kujitetea Machi 14 na 19, hivyo nataka upande wa utetezi mje na mashahidi hao kwa muda tuliopanga ili kesi hii iweze kuisha mapema kabla mwezi Machi haujaisha" alisema Simba.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527