RAIS MUSEVENI APIGA MARUFUKU KUWATUMIA WANAWAKE WENYE MAKALIO MAKUBWA KUVUTIA WATALII

Rais wa Uganda Yoweri Museveni amesema hataruhusu mwanamke hata mmoja kutoka nchini humo kuonyesha mwili wake kwa umma kama njia moja ya kuwavutia watalii.

 Akiwa kwenye mkutano na wawekezaji katika Ikulu Alhamisi Februari 7,2019 Museveni alilaani pendekezo hilo la kutaka kuwatumia wanawake wenye makalio makubwa kama kivutio cha utalii. 

Museveni alidai kuwa pendekezo hilo lililotolewa na waziri wa Utalii Godfrey Kiwanda halikuwa limejadiliwa na baraza la mawaziri  huku akitaka wanawake waheshimiwe.


Aidha, Rais Museveni pia alisema hakuna uhakika kwamba wanawake kuonyesha makalio yao itavutia watalii Uganda.

 "Huu haukuwa uamuzi wa baraza la mawaziri, watu hawapaswi kuja hapa kuona wanawake, sijafurahishwa na pendekezo hilo hata kidogo. Hiyo ni kama kuwauza wanawake wetu kwa watalii," Museveni alisema.

 Museveni pia alisema wanawake wanapaswa kuheshimiwa na kushughulikiwa ipasavyo ila sio kuwaanika mitandaoni kama njia moja ya kuwauza.

 "Lazima tujipe muda wa kujadili suala hili, niko na maoni yangu binafsi na tayari nishayazungumzia, siwezi wakubali wajukuu wangu kuonyesha miili yao kwa umma eti kwa ajili ya kukuza utalii, ningependa tumtumie Abenakyo, Miss World Africa kuuza Uganda kwa mataifa mengine," Museveni aliongezea.

Mapema mwezi huu, Wizara ya Utalii nchini Uganda ilikuwa imetangaza kuwa itawatumia wanawake wenye makalio makubwa kama kivutio cha utalii. 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527