SERIKALI YATANGAZA KUZIMA INTANETI ILI KUJILINDA NA MAADUI

Serikali ya Urusi chini ya Rais Vladimir Putin inajipanga kuzima mtandao wa intaneti kwa muda, na hivyo kujitoa kwenye mawasiliano na dunia kama sehemu ya majaribio yake ya kujikinga dhidi ya mashambulio ya kimtandao.

Zoezi hilo litafanya mawasiliano baina ya raia na mashirika ya Urusi kubaki ndani ya nchi badala ya ya kupitia njia za kawaida za kimtandao kimataifa.

Rasimu ya sheria ya kuruhusu mabadiliko ya kiufundi ili kuiwezesha nchi hiyo kuendesha mtandao wake wenyewe iliwasilishwa bungeni mwaka jana.

Jaribio hilo linatarajiwa kufanyika kabla ya tarehe mosi Aprili, lakini siku rasmi ya kuzimwa mtandao haijatajwa.

Mvurugano mkubwa

Rasimu hiyo ya sheria, iliyopewa jina la Programu ya Taifa ya Uchumi wa Kidijiti, inawataka watoa huduma za intaneti nchini Urusi kuwa na uwezo wa kuendelea na huduma zao hata pale ikitokea nchi za kigeni zikiamua kuitenga Urusi.

Nchi wanachama wa Nato na washirika wake wamekuwa wakitishia kuiwekea vikwazo vya kimtandao Urusi ambayo wanaituhumu kwa kufanya mashambulio ya kimtandao.

Njia mojawapo inayopangwa na Urusi katika kujilinda huko ni kutengeneza mfumo wake binafsi wa anuani za kimtandao ufahamikao kama DNS, waweze kupata mawasiliano hata pale watakapotengwa ama kujitenga.
Kwa sasa, kuna taasisi 12 zinzoshughulikia suala la utolewaj na matumizi ya anuani hizo na hakuna hata moja iliyopo Urusi.

Hata hivyo tayari kuna chapa nyingi za mfumo huo wa DNS nchini Urusi hali inayoonesha kuwa nchi hiyo inaweza kuendelea na shughuli zake za kimtandao hata ikitokea imetengwa leo.

Watoa huduma za intaneti wanatarajiwa kuelekeza mawasiliano yote yanayopita kwao kwenye vituo vya serikali kwenye zoezi hilo. Mawasiliano yote ya ndani ya Urusi yataruhusiwa kuendelea lakini yale yatokayo nje ya nci yataminywa.

Mwishowe, serikali ya Urusi itakuwa na ubavu kama wa China wa kupanga mawasiliano gani raia wake wapate kutoka nje ya nchi.

Vyombo vya habari nchini humo vinadai kuwa watoa huduma za intaneti nchini humo wanakubaliana na mabadiliko hayo lakini wanatofautiana kwenye namna gani utekelzwaji wake uwe. Wanaamini jaribio hilo litazaa "mvurugano mkubwa" kwa matumizi ya mtandao ya nchi hiyo, umeandika mtandao wa ZDNet.
Serikali ya Urusi inawapa fedha watoa huduma ya intaneti nchini humo ili kuboresha miundombinu yao kuendana na mipango yake ya baadae.

Hata hivyo, kuna uwezekano wa watu kuchupa mazuio hayo ya serikali kwa kutumia mitandao binafsi (VPNs) - ambayo hudanganya mahala kompyuta ama simu janja ilipo na hivyo vidhibiti kushindwa kuzizui kupata mawasiliano yaliyokatazwa.

Hata hivyo, baadhi ya nchi kama China zimekuwa wakali kwa wale wanaotumia tenkolojia hiyo. Ukikutwa unatumia ama kusambaza bila kibali teknolijia hiyo nchini China unaweza kutupwa jela.

Mara chache, nchi hujikuta zimejitoa kwenye mawasiliano ya intaneti kwa bahati mabaya - ilitokea hivyo mwaka 2018 nchini Mauritania kwa siku mbili baada ya nyaya ya chini ya bahari inayopeleka mawasiliano hayo kukatika. Meli ya kuvua samaki inasadikiwa kusababisha ajali hiyo.

Chanzo- BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527