WATUMISHI 9 WIZARA YA ARDHI WAFARIKI KWA AJALI GARI KUTUMBUKIA MTONI


 
Watumishi tisa kati ya 13 wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wamefariki dunia katika ajali ya gari.

Ajali hiyo imetokea Jumamosi Februari 23, 2019 saa 11 jioni baada ya gari hiyo mali ya Serikali STK 9444 kutumbukia mto Kikowila uliopo katikati ya Kiberege na Mji wa Ifakara wilayani Kilombero mkoani Morogoro.

Watumishi hao 13 waliokuwa kwenye gari hiyo aina ya Land Cruiser walikuwa wakitoka kwenye shughuli za upimaji ardhi zinazoendelea wilayani humo.

Manusura wa ajali hiyo wamelazwa hospitali ya St. Francis mkoani Morogoro kwa matibabu

TANZIA

"Nimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya ajali ya gari la Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero iliyotokea jioni ya leo huko Ifakara. Katika ajali hiyo watu tisa wamepoteza maisha na wengine wanne wamejeruhiwa.

Gari hilo lilikuwa limewabeba watumishi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi waliokuwa wameajiriwa na Mradi wa Kuwezesha Umilikishaji wa Ardhi ( Land Tenure Support Programme -LTSP). Watumishi hao walikuwa wanatoka katika Kijiji cha Kibegere kurudi Ifakara ambako walikwenda huko kikazi. Ajali hiyo imepoteza nguvu kazi ya taifa kwa vile wengi wao walikuwa vijana. 

Kwa niaba ya serikali na watumishi wa Wizara ya Ardhi, kwa masikitiko makubwa, nawapa pole wafiwa wote wazazi, ndugu, jamaa na marafiki kwa kuondokewa na wapendwa vijana wetu na ninawathibitishia kuwa serikali inafanya kila iwezalo kuokoa misha ya majeruhi na kuhakikisha miili ya marehemu wote inasafirishwa na kuzikwa kwa mujibu wa taratibu.

Namuomba Mwenyezi Mungu atutie nguvu katika kipindi hiki kigumu na awajalie majeruhi wapone haraka na roho za marehemu zipate pumziko la milele. Amen"

William V. Lukuvi 

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527