WALIMU,WANAFUNZI WAFIKISHWA MAHAKAMANI KWA WIZI WA MITIHANI KIDATO CHA NNE 2018

Watu18 akiwemo mkuu wa shule ya Shule ya Sekondari Tumaini Lutheran Seminary iliyopo wilayani Malinyi, Mkoa wa Morogoro, baadhi ya walimu, wasimamizi wa mitihani na baadhi ya wanafunzi wamefikishwa katika mahakama ya Wilaya ya Ulanga wakikabiliwa na makosa yanayohusu udanganyifu wa mitihani ya kidato cha nne.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Willbroad Mutafungwa alibainisha hayo jana wakati akizungumzia hatua ambazo zimechukuliwa na polisi kutokana na sakata la wizi wa mitihani ya kidato cha nne 2018.

Sambamba na washitakiwa hao raia kufikishwa mahakamani, Kamanda Mutafungwa amesema pia wamemtia mbaroni askari mwenye namba G 7281 Konstebo Khamisi na kumfikisha mahakama ya kijeshi kufuatia tuhuma za kujihusisha kwake, kushiriki kwa kupanga njama na kufanya udanganyifu wa mitihani wa kidato cha nne wa shule hiyo.

Alibainisha kuwa askari huyo kulingana na kanuni za jeshi atafikishwa kwanza katika mahakama ya kijeshi ili taratibu nyingine ziweze kuchukuliwa na baada ya hapo atafikishwa mahakama ya kiraia kwa mujibu wa sheria za nchi.

Kwa sasa wilaya ya Malinyi bado haina mahakama ya wilaya ambapo mashauri yake yanayohusiana na ngazi ya mahakama ya wilaya yanashughulikiwa na Mahakama ya Wilaya ya Ulanga.

Hivi karibuni Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), Dk Charles Msonde akizungumza Dodoma na waandishi wa habari wakati akitangaza matokeo ya kidato cha nne 2018 alisema baadhi ya wanafunzi wa shule mbalimbali walifutiwa matokeo kutokana na kubainika kufanya udanganyifu kwa kuingia na notes ( nondo), kwenye chumba cha mtihani.

Dk Msonde amesema katika hali ya kusikitisha, uongozi wa sekondari hiyo yenye namba za usajili S0983, ulionekana kupanga mbinu za ushindi kwa kuandaaa miundombinu ya kufanya udanganyifu, jambo lililolifanya Baraza la Mitihani Tanzania kufuta matokeo ya wanafunzi 57.

Via Habarileo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527