PROF. MBARAWA AONGOZA ZOEZI LA KUPANDA MITI 600 MJI WA SERIKALI DODOMA



Watumishi wa Wizara ya Maji wamepanda miti katika eneo la Ihumwa kwenye mji wa serikali zoezi lililoongozwa na Waziri wa Maji Profesa Makame Mbarawa.

Jumla ya miti 600 imepandwa na watumishi wa Wizara pamoja na viongozi akiwemo Katibu Mkuu Profesa Kitila Mkumbo, Naibu Katibu Mkuu, Mhandisi Emmanuel Kalobelo, Wakurugenzi na Wakuu wa Vitengo.

Profesa Mbarawa ameelekeza teknolojia ya kisasa ya umwagiliaji itumike ili miti yote ilipandwa ikue. Amesema kuwa zipo teknolojia mbali mbali za umwagiliaji ambazo wataalamu wetu wanatakiwa kuzijua na kuzitumia.

Zoezi la upandaji miti kwenye kiwanja cha Wizara liliwahusisha wataalamu wa misitu kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) ambayo imetoa miti hiyo ikiwa ni kampeni ya kulifanya jiji la Dodoma kuwa kijani.

Awali, Naibu Katibu Mkuu, Mhandisi Kalobelo alisema kuwa, tayari Wizara ya Maji ina kisima kitakachotumika katika umwagiliaji wa miti na bustani za wizara hivyo miti iliyopandwa itatunzwa kama inavyotakiwa.

Jumla ya watumishi 300 walishiriki zoezi la upandaji miti katika mji wa Serikali - Ihumwa kwenye kiwanja cha Wizara.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527