SERIKALI YAKANUSHA KIKUNDI KUITISHIA TANZANIA

Kwa siku kadhaa za hivi karibuni kumekuwa na taarifa inayosambaa kwa njia ya video ambayo inaonesha kikundi cha watu wakiwa wameketi, wakitumia lugha ya Kiswahili kutishia kuvamia na kushambulia baadhi ya nchi kadhaa za Afrika Mashariki ikiwemo Tanzania.


Taarifa ya Msemaji Mkuu wa Serikali imesema, "baada ya uchunguzi wetu tumebaini ilirushwa mwaka 2016 na Kituo cha Televisheni cha China (CCTV-Afrika), ikielezea hisia za uwepo wa viashiria vya kundi la Al-Shaabab nchini Tanzania.

Imeendelea kusema taarifa hiyo kuwa, msingi wa taarifa hiyo ya mwaka 2016 ni ripoti yenye kurasa 53 iliyoandaliwa na wataalamu wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Mashariki mwa Afrika (IGAD), ambayo hata hivyo haikujikita kwenye utafiti wowote wa moja kwa moja kuhusu Tanzania bali hisia za watu na makundi mbalimbali katika nchi za Kenya, Ethiopia na Somalia.

"Tumewasiliana na wamiliki wa CCTV-Afrika na wamekiri kuwa sio wao walioisambaza tena video hiyo, ikionekana dhahiri kuwa kuna watu wenye nia mbaya na nchi yetu wameitumiavideo hiyo ya mwaka 2016 kwa malengo yao hasi dhidi ya Tanzania".

Serikali imesema kuwa kwa kushirikiana na CCTV yenyewe inawataka wananchi kupuuzia taarifa zozote zenye lengo la kuipaka matope Tanzania na kuihusisha na kundi lolote la kigaidi.

Pia serikali imeusisitizia umma kuwa Tanzania iko salama, na vyombo vyake vya ulinzi na usalama viko makini kufuatilia na kuchukua hatua iwapo kuna viashiria vyovyote vya kuharibu amani.
Chanzo : Eatv

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527