MKURUGENZI AZITAKA YANGA NA SIMBA KUTODHARAU MICHUANO YA SPORTPESA

Michuano ya SportPesa Super Cup mwaka 2019, inatarajia kuzinduliwa leo katika Uwanja wa Taifa Jijini Dar es salaam kwa michezo miwili kupigwa.

Mchezo wa kwanza wa leo utakuwa ni kati ya Singida United na Bandari ya Kenya, majira ya saa 8:00 mchana huku Yanga ikiwakaribisha Kariobang Sharks ya hukohuko Kenya huku katika mchezo wa pili wa saa 10:00 jioni.

Kuelekea ufunguzi wa michuano hiyo, Mkurugenzi wa Uendeshaji wa SportPesa nchini, Abbas Tarimba, amevitaka klabu za Simba na Yanga kutumia vikosi vya kwanza ili kuepusha aibu ambayo imekuwa zikiionesha katika misimu miwili iliyopita.

"Imekuwa ni utamaduni wetu, Samahani nitatumia neno 'kudharau' haya mashindano, awamu hii hatutaki utani, tunataka kombe libaki nyumbani kwa maana kila siku limekuwa likienda nchi jirani. Tunavitaka vilabu vyote vya hapa nyumbani kuhakikisha vinafanya vizuri", amesema Tarimba.

"Nilivyokuwa naingia hapa nilikutana na kocha wa Yanga, nikamsisitiza kuwa hatutaki utani katika mashindano ya mwaka huu", ameongeza.

Awali, michuano hii ilikuwa ikifanyika mwezi Juni baada ya ligi kumalizika lakini Tarimba amesema kuwa imekuwa ikilalamikiwa na vilabu hasa vya Tanzania kuwa inapofika mwishoni mwa msimu, wachezaji wengi mikataba yao huwa inamalizika kwahiyo kukosa fursa ya kushiriki. 

Pia ameitaja sababu nyingine kuwa ni klabu hizo kutokuwa na muda mrefu wa maandalizi kutokana na ligi kumalizika, tofauti na timu za Kenya ambazo katika kipindi hicho ligi yao inakuwa inaendelea.

Mshindi wa michuano hiyo atajinyakulia kitita cha Dola za Kimarekani 30,000 ambazo ni takribani shilingi milioni 65 za Kitanzania, huku mshindi wa pili akijinyakulia Dola 10,000, wa tatu atapata Dola 7,500 na mshindi wa nne atapata Dola 5,000.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527