Picha : NAIBU WAZIRI MWITA WAITARA AFANYA ZIARA SHINYANGA KUKAGUA MIRADI YA AFYA,ELIMU..ABAINI MADUDU

Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara, amefanya ziara mkoani Shinyanga kwa kukagua ujenzi wa miradi ya maendeleo kwenye sekta ya afya na elimu katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga na manispaa ya Shinyanga, na kubaini kuwepo na ubadhirifu wa fedha kwenye ujenzi wa shule Shikizi kwenye halmashauri zote mbili.


Waitara amefanya ziara hiyo leo Desemba 4,2018 ambapo alianza kwa kuzungumza na watumishi wa Serikali wa halmashauri zote mbili katika ofisi ya mkuu wa wilaya ya Shinyanga na kutoa maagizo kwao kufanya kazi kwa bidii pamoja na kuthamini fedha ambazo hutolewa kwa ajili ya ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Baada ya kutoa maagizo hayo kwa watumishi wa Serikali, alianza kufanya ziara kwa kukagua ujenzi wa hospitali ya wilaya ya Shinyanga wenye thamani ya Shilingi Bilioni 1.5 ambao mpaka sasa umeshatumia Shilingi Milioni 500 na kuagiza ujenzi wake ukamilike haraka ili wananchi waanze kupata matibabu maeneo ya karibu.

Mradi mwingine aliotembelea ni ule wa ujenzi wa Shule Shikizi Mwabuki Kata ya Solwa Halmashauri ya Shinyanga, ndipo alipoanza kubaini kuwepo na ubadhirifu wa fedha kwenye miradi ya shule hizo baada ya kukuta kuna ujenzi wa jengo moja lenye vyumba viwili vya madarasa pamoja na vyoo viwili, huku fedha iliyotumika haiendani na thamani ya ujenzi wake.

Alisema fedha zilizotumika kwenye ujenzi wa shule hiyo Shikizi ambazo ni Shilingi Milioni 45 haziendani kabisa na thamani ya fedha hizo.

“Miradi yote ya ujenzi wa shule shikizi katika halmashauri ya Shinyanga pamoja na manispaa ya Shinyanga sijaridhika na fedha ambazo zimetumika kwenye ujenzi wake bali nahofia kuwepo na ubadhirifu wa fedha, hivyo nawaomba wakurugenzi wote nipate taarifa juu ya miradi hii, hapa kuna fedha lazima zimeliwa,”alisema Waitara.

“Haiwezekani fedha zote hizi zijenge Jengo moja tu lenye madarasa mawili, kwa kila Shule Shikizi, Mwabuki zimetumika Milioni 45, Mwamagulya Milioni 58, pamoja na Lyandu Milioni 60, lakini katika Zahanati ya Solwa zimetumika milioni 38 kwa kujenga majengo mawili tena makubwa, hapa lazima fedha zimetafunwa, naagiza uchunguzi ufanyika na nipewe taarifa”,aliongeza.

Pia ameagiza ujenzi wa miradi hiyo ya Shule Shikizi, uwe unashirikisha wananchi wa maeneo husika kwa kuchangia nguvu kazi pamoja na kuwepo kwenye kamati za ujenzi, manunuzi na mapokezi, ili kuondoa vitendo vya ubadhirifu wa fedha.


Nao wakurugenzi wote wa halmashauri hizo mbili Geofrey Mwangulumbi wa manispaa ya Shinyanga pamoja na Hoja Mahiba wa halmashauri ya Shinyanga , kwa nyakati tofauti wote walikiri kutii magizo ya naibu waziri huyo kwa kutuma wakaguzi wa ndani (CAG), ili kufanya uchunguzi wa ubadhirifu wa fedha kwenye miradi hiyo ya Shule Shikizi.

Kwa upande wake Mwangulumbi alisema yeye tayari alishatuma mkaguzi wa ndani (CAG) kufanya ukaguzi kwenye miradi hiyo ya Shule Shikizi wa Mwamagulwa pamoja na Lyandu, mara baada ya kuona fedha zilizotumika haziendani na idadi ya majengo.


TAZAMA PICHA HAPA CHINI
Wa pili kushoto ni Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akiwa ameambatana viongozi mbalimbali akifanya ziara katika halmshauri ya wilaya ya Shinyanga.Wa kwanza kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Jasinta Mboneko,wa tatu ni Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Azza Hilal Hamad akifuatiwa na Mganga mkuu wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga  Amos Mwenda.Picha zote na Marco Maduhu - Malunde1 blog


Naibu waziri Ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akikagua wodi katika ujenzi wa hospitali ya wilaya ya Shinyanga ambazo zilijengwa chini ya kiwango na kuagiza zibomolewe.
Mganga mkuu wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Dkt. Amos Mwenda akimuonyesha ramani ya ujenzi wa hospitali ya wilaya ya Shinyanga Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara.
Mganga mkuu wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Amos Mwenda akitoa maelezo namna ujenzi wa hospitali ya wilaya hiyo unavyokwenda ambapo mpaka sasa wameshapokea shilingi Milioni 500 kutoka Serikalini na ujenzi wake utagharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 1.5 ambapo mwakani wanaweza pia kuanza kutoa matibabu huku wakiendelea kukamilisha ujenzi wodi polepole.
Baadhi ya akina mama wakimsikiliza Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akisisitiza ujenzi wa hospitali ya wilaya hiyo ya Shinyanga ukamilike mapema ili wananchi waanze kupata huduma za matibabu karibu.
Wananchi wakiendelea kumsikiliza Naibu Waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara juu ya msisitizo wa ujenzi wa hospitali ya wilaya hiyo, wakiwa na Makamu mwenyekiti wa halmshauri ya wilaya ya Shinyanga Isack Sengerema (wa kwanza kushoto).
Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akikagua ujenzi wa wodi katika Zahanati ya Solwa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga, ambapo mpaka sasa umegharimu kiasi cha Shilingi Milioni 38.
Ziara ya ukaguzi wa majengo ya Wodi katika Zahanati ya Solwa ikiendelea.
Diwani wa Kata ya Solwa Awadhi Abood akifurahia jambo na Mbunge wa viti maalumu mkoa wa Shinyanga Azza Hilal wakati wa ziara hiyo ya Naibu Waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara katika ukaguzi wa wodi kwenye Zahanati ya Solwa.
Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akikagua ujenzi wa shule Shikizi ya Mwabuki iliyopo katika kata ya Solwa kwa ajili ya kusomea wanafunzi wa utayari ili kuwapunguzia adha ya umbali mrefu wa shule na kubaini kuwapo na ubadhirifu wa fedha.
Naibu Waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akielezea kusikitishwa na namna fedha za Serikali zinavyotumiwa hovyo na watumishi wa umma kwa kutosimamia miradi vizuri ya maendeleo na kuishia kutafuna pesa bila hata ya kuogopa ukali wa Rais Magufuli.
Moja ya choo kikionekana kilivyojengwa madirisha yake katika shule hiyo Shikizi ya Mwabuki na kuagiza yajengwe upya.
Naibu waziri Ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akiagiza mhandisi ambaye amesimamia ujenzi katika shule hiyo Shikizi awekwe chini ya ulinzi na ukaguzi ufanyike kwenye mradi huo ikiwa amekula fedha kwani ujenzi wake hauendani na fedha iliyokwisha kutumika.
Mhandisi wa ujenzi katika halmashauri hiyo ya wilaya ya Shinyanga Hassani Mwanri, akijitetea kwa Naibu waziri huyo Mwita Waitara kuwa yeye ni mgeni hivyo ujenzi wa majengo hayo ya Shule Shikizi ameyakuta yameshajengwa tayari.
Ziara ikiendelea ya ukaguzi katika Shule Shikizi ya Mwamagula manispaa ya Shinyanga ,ambapo ujenzi wa jengo moja lenye madarasa mawili likiwa limesha gharimu kiasi cha Shilingi Milioni 58, na kumfanya Naibu Waziri Waitara kuingiwa na mashaka kuwa fedha za mradi huo zimetafunwa ikiwa idadi ya majengo hailingani na fedha husika.
Ziara ya ukaguzi wa shule Shikizi ikiendelea.
Naibu Waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akiendelea na ziara ya kukagua ujenzi wa Shule Shikizi Lyandu Kata ya Kizumbi manispaa ya Shinyanga ambao nao umeshagharimu Shilingi Milioni 60 kwa ujenzi wa jengo moja lenye madarasa mawili na vyoo viwili, na hivyo kuagiza ukaguzi wa miradi hiyo yote ufanyike na kupewa taarifa sahihi.
Wananchi katika kijiji cha Lyandu Kata ya Kizumbi manispaa ya Shinyanga wakimpokea Naibu Waziri huyo Mwita Waitara na kuipongeza Serikali wa ujenzi wa Shule hizo Shikizi ambazo zitawasaidia watoto wao wadogo kuwapunguzia adha ya kusoma umbali mrefu.
Mwananchi wa kijiji cha Lyandu Shija Tungu naye akipongeza Serikali kwa ujenzi wa shule hizo Shikizi ambazo zimekuwa msaada kwa watoto wao kupata elimu.
Naibu Waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akizungumza na wananchi wa Lyandu na kuwataka waendelee kuchangia shughuli za maendeleo.

Mkurugenzi wa manispaa ya Shinyanga Geofrey Mwangulumbi akielezea namna walivyoanza kuchukua hatua juu ya ujenzi wa miradi hiyo ya Shule Shikizi ambapo tayari ameshamtuma mkaguzi wa ndani kufanya uchunguzi juu ya matumizi ya fedha.
Awali Naibu Waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akiteta jambo na mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko kabla ya kuongea na watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga vijijini na Manispaa.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akimkaribisha Naibu waziri Waitara kuzungumza na watumishi wa halmashauri mbili za Shinyanga na Manispaa.
Naibu waziri Ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akizungumza na watumishi wa halmashauri hizo na kuwataka wafanye kazi kwa bidii,kujituma pamoja na kusimamia fedha za miradi ya maendeleo sabamba na kutoa fedha asilimia 10 kwa akina mama,vijana na walemavu.
Watumishi wa Serikali wakisikiliza maagizo mbalimbali kutoka kwa Naibu waziri Waitara na kutakiwa fedha za mapato ya ndani asilimia 40 wazielekeze kwenye ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo.
Awali Mbunge wa viti maalumu mkoani Shinyanga Azza Hilal akizungumza kabla ya ziara kuanza na kumuomba naibu waziri huyo kusaidia fedha za ujenzi wa makao makuu ya halmashauri ya wilaya ya Shinyanga ,ili watumishi wawe karibu na wananchi na waweze kupata huduma stahiki kuliko hivi sasa ofisi za halmashauri hizo zipo mjini Shinyanga.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akimkaribisha Naibu waziri Waitara mjini Shinyanga tayari kwa ziara yake ya kikazi.
Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akisalimiana na katibu tawala wa wilaya Boniphace Chambi alipowasili mjini Shinyanga tayari kwa ziara yake ya kikazi.
Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akisalimiana mbunge wa vitimaalumu mkoani Shinyanga Azza Hilal alipowasili mjini Shinyanga kwa ziara yake ya kikazi.
Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akisalimiana katibu wa CCM Wilaya ya Shinyanga mjini Charles Sangula alipowasili mjini Shinyanga kwa ziara yake ya kikazi.
Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akisalimiana mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Ngassa Mboje, alipowasili mjini Shinyanga kwa ziara yake ya kikazi.
Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akisalimiana na Mkurugenzi wa manispaa ya Shinyanga Geofrey Mwangulumbi alipowasili mjini Shinyanga kwa ziara yake ya kikazi.
Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Mwita Waitara akisalimiana na Kamati ya Ulinzi na usalama alipowasili mjini Shinyanga kwa ajili ya ziara yake ya kikazi.

Picha zote na Marco Maduhu- Malunde1 Blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527