REPSSI WAANZA KAMPENI KUPAMBANA NA MIMBA NA NDOA ZA UTOTONI


Mkurugenzi mkazi wa taasisi inayojishughulisha na maswala ya kisaikolojia (RESPSSI) Tanzania,Edwick Mapalala akizungumza wakati wa kampeni ya kutokomeza tatizo la ndoa na mimba za utotoni
Mkurugenzi mkazi wa taasisi inayojishughulisha na maswala ya kisaikolojia (RESPSSI) Tanzania,Edwick Mapalala akizungumza wakati wa kampeni ya kutokomeza tatizo la ndoa na mimba za utotoni
Baadhi ya vijana wa boda boda waliochangia mjadala wa kupinga ndoa na mimba ya utotoni

Shirika lisilo la Kiserikali linalojihusisha na masuala ya
Kisaikolojia nchini (REPPS) limeanza kufanya kampeni ya kupambana na tatizo la mimba na ndoa za utotoni baada ya tafiti nyingi kuonyesha bado tatizo hilo ni
kubwa.

Takwimu za Democratic and Health Survey , zinaonyesha kuwa tatizo la mimba za utotoni nchini limeongezeka kutoka asilimia 23 mwaka 2010 hadi kufikia 27 mwaka 2016/17, kutokana na ukosefu wa huduma pamoja na elimu ya afya ya uzazi kwa vijana wenye
umri kuanzia miaka 15 hadi 19.

Mkurugenzi Mkazi wa Repps, Tanzania Edwick Mapalala amesema kampeni hiyo wanaiendesha kwa kuzungumza na jamii kwenye vijiwe, shambani, maeneo ya masomo na mikusanyiko
yote ili kufikisha elimu ya namna ya kuwalea na kuwatunza watoto kimaadili.

“Tatizo la mimba na ndoa za utotoni lipo kwenye jamii yenyewe, wazazi na walezi wakijua umuhimu wa malezi bora tatizo hili halitakuwepo kabisa,” amesema.

Amesema kama watoto wa kike wataendelea kukatisha masomo yao kwa mimba na ndoa itakuwa vigumu kufikia ndoto ya Tanzania yenye viwanda kwa sababu nguvu kazi inayoachwa njiani ni kubwa.

“Mtoto wa kike akipata elimu na kusoma kwa bidii atatimiza ndoto yake na kuja kuchangia maendeleo kwenye taifa lake,” amesisitiza.

Amesema kupitia kampeni hiyo wanayoiendesha kwa ushirikiano na Shirika lililo chini ya Kanisa la Roman Katoliki jimbo kuu la Dar es Salaam (PASADA), vijana wameweza kupewa
elimu ya afya ya uzazi na kujitambua itakayowasaidia kufikia ndoto zao.

Kaimu Afisa Mtendaji wa kijiji cha Parang’andam Felisian Magulu amesema kupitia kampeni hizo jamii inapata ufahamu wa madhara ya mimba kwa watoto na kujua namna ya kupambana na tatizo hilo.

Naye Mwenyekiti wa kijiji cha Mkuranga, Dunia Mabufu alikiri kuwepo kwa kampeni za aina hiyo kunasaidia katika kubadilisha fikra za wengi zinazoendeshwa na mila na desturi
kandamizi dhidi ya wasichana na wanawake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527