MWALIMU AFUKUZWA KAZI KISA KAMNYOA NYWELE MWANAFUNZI DARASANI...HATARINI KUTUPWA JELA


Mwalimu mmoja nchini Marekani anakabiliwa na mashtaka ya uhalifu, baada ya picha ya video kusambaa mitandaoni akimkata kwa lazima nywele mwanafunzi mmoja darasani, huku akiimba wimbo wa taifa wa Marekani.

Margaret Gieszinger, 52, amefukuzwa kazi kwa kitendo hicho alichokifanya katika Shule ya Sekondari ya Chuo Kikuu cha huko Visalia, California.

Waendesha mashtaka wamesema kuwa amekanusha makosa sita dhidi yake, likiwemo kosa la ukatili dhidi ya mtoto na shambulio la kimwili. Anakabiliwa na hukumu ya miaka mitatu unusu jela iwapo atakutwa na hatia.

Bi Gieszinger, aliachiliwa kwa dhamana ya dola 100,000 Ijumaa jioni.

Katika video hiyo ya iliyochukuliwa kwa simu ya mkononi kisha kupakiwa kwenye mtandao wa Reddit, mwalimu huyo anayefunza somo la sayansi, anaonekana akimuita mwanafunzi wa kiume kuketi mbele ya darasa, kisha akaanza kumkatakata nywele huku akiimba kwa makosa wimbo wa taifa la Marekani maarufu kama Star Spangled Banner.

Wakili wa mwanafunzi huyo, ameliambia shirika la habari la CNN kuwa, mteja wake "alishtuka sana" kabla ya kufanikiwa kujinasua mikononi mwa mwalimu huyo.

Bi Gieszinger kisha anaonekana kwenye video, akishika mkasi mkononi juu ya kichwa chake na kusema "next!" yaani "mwingine!" na kutishia pia kumkata nywele mwanafunzi mmoja wa kike.

"Tunachukulia kwa tahadhari kubwa mno usalama wa wanafunzi madarasani," hiyo ni kwa mjibu wa taarifa kutoka kwa afisi kuu ya Elimu ya kaunti ya Tulare.

"Tunachunguza taarifa zote tunazozipokea na tutachukua hatua kali mno na zinazohitajika dhidi ya wafanyakazi wetu walio na utovu wa nidhamu." Taarifa hiyo imeongeza.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527