BABA AUA WATOTO WAKE WATATU KWA SUMU KISA MGOGORO NA MKEWE

Mkazi wa Kijiji cha Kunke wilayani Mvomero, Mkoa wa Morogoro, Salehe Masokola (22), amewaua watoto wake watatu kwa kuwanywesha sumu.

Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani, Wankyo Nyigesa, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na alisema lilitokea Novemba 27, mwaka huu saa sita mchana katika maeneo ya Kibindu, Halmashauri ya Chalinze mkoani Pwani.

Kamanda Nyigesa, alisema mtuhumiwa huyo alikuwa na mgogoro na mke wake na wakati ukitokea watoto walikuwa wakiishi Kunke kwa mama mkwe wake.

Alisema baada ya mgogoro huo, mtuhumiwa huyo alisafiri hadi kwa mkwewe na kuwachukua watoto hao kwa kisingizio cha kutaka kwenda kucheza nao kisha baadaye angewarudisha.

Alisema baada ya maelezo hayo, mtuhumiwa huyo aliwapakia watoto hao katika baiskeli kutoka Kunke hadi Kitongoji cha Ditele Kibindu, Chalinze na aliwanywesha sumu ya twiga amine ambayo ni dawa ya kuulia magugu iliyopoteza maisha yao.

“Masokola alichukua sumu hiyo na kisha kuwachanganyia katika juisi na kuwanywesha watoto hao na kusababisha kupoteza maisha yao papo hapo na katika eneo la tukio tuliokota chupa mbili za juisi zilizotumika, chupa ya dawa na matapishi ambavyo vilichukuliwa kwa uchunguzi zaidi,” alisema.

Alitaja majina ya watoto waliofariki katika tukio hilo kuwa ni Shaila Salehe (6), Nurdin Salehe (4) na Sabrat Salehe aliyekuwa na umri wa miezi 10.

Pia alisema baada ya mtuhumiwa kufanya tukio hilo na yeye aliamua kunywa sumu kwa lengo la kutaka kujiua lakini ilishindikana kwa kuwa aliokolewa na wasamaria wema na kisha kukimbizwa katika Hospitali ya Mission ya Bwagala iliyopo Mvomero kwa matibabu lakini hali yake bado ni mbaya akiwa katika chumba cha wagonjwa mahututi chini ya uangalizi wa Jeshi la Polisi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527