WAITARA: BARABARA MBOVU ZISINGOJE ZIARA YA KIONGOZI NDIO ZIFANYIWE MATENGENEZO

WAKALA wa Barabara za Vijijini na Mijini nchini (TARURA) ameagizwa kuhakikisha barabara zote zilizo chini yao zinapitika wakati wote na sio kusubiri viongozi waje ndio zifanyiwe matengenezo.

Kauli hiyo imetolewa hivi karibuni na Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali (OR TAMISEMI) Mwita Waitara mara baada ya kutembelea miradi mbalimbali na kukutana barabara zinakwenda katika miradi hiyo ziko katika hali isiyoridhisha.

Alisema ubora wa barabara sio kwa ajili ya viongozi pekee bali zinatakiwa kuwasaidia wananchi katika kujiletea maendeleo na kuchangia katika ujenzi wa uchumi wa viwanda.

Waitara alisema kuwa barabara ni lazima ziwasaidie wakulima kutoa mazao yao mashambani na kufikisha katika sehemu husika au sokoni kirahisi.

“Barabara lazima ziwe rafiki wakati wote kuwawezesha wananchi kwenda kupata huduma za matibabu kirahisi, wanafunzi kufika shule kirahisi na wakulima kutoa mazao yao mashambani bila vikwazo…barabara zinapitika sio kwa ajili ya viongozi bali ni kwa ajili ya wananchi wote…TARURA lazima muhakikishe barabara zenu zinapitika wakati wote” alisema.

Waitara aliongeza kuwa TARURA wamepewa jukumu la kuhakikisha wanasimamia barabara za vijiji na mijini wakati wanapokuwa ni lazima akili na nguvu zao wazielekeze katika kuboresha barabara.

“Kazi yenu ni barabara …mnapokuwa Ofisini ni barabara…mnapolala wazeni barabara…mnapoamka ni barabara…kila mnapofanyakazi fikirieni barabara ndio kazi mliopewa”alisisitiza.

Alisema urahisi wa usafiri unaotokana na ubora wa barabara hasa za vijijini utasaidia kuharakisha malighafi kufika viwandani na masokoni na hivyo kuinua pato la mwananchi na maendeleo ya nchi.
NA TIGANYA VINCENT,TABORA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527