Picha : AGAPE YAKUTANISHA WANAFUNZI 400 USANDA KWENYE KONGAMANO LA ELIMU YA AFYA YA UZAZI NA UJINSIA

Shirika la Agape la Mjini Shinyanga limefanya Kongamano kwa wanafunzi 400 wa shule za msingi na sekondari katika kata ya Usanda halmashauri ya wilaya ya Shinyanga kwa lengo la kutoa elimu kuhusu afya ya uzazi na ujinsia ili kukabiliana na mimba na ndoa za utotoni. 

Kongamano hilo lililohudhuriwa na wanafunzi wa shule nane zilizopo katika kata hiyo,limefanyika katika Uwanja wa Kijiji cha Singita ambapo mgeni rasmi alikuwa Kaimu Afisa Elimu wa Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga,Mary Maka. 

Wanafunzi waliohudhuria kongamano hilo ni kutoka shule za msingi Nzagaluba, Manyada, Busanda, Shabuluba pamoja na Shingida ambapo za sekondari ni Samuye, Usanda na Shingita. 

Kongamano hilo lililoanza kwa maandamano lilienda sanjari na Mdahalo wenye mada ‘Nini Manufaa/faida ya elimu ya afya ya uzazi na ujinsia’ pia lilitawaliwa na michezo na burudani mbalimbali kutoka kwa wanafunzi hao vyote vikilenga kutokomeza mimba na ndoa za utotoni. 

Akizungumza wakati wa Kongamano hilo, Afisa Elimu wa Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga,Mary Maka aliwataka wanafunzi kuzingatia masomo yao na kuwa na hofu ya Mungu ili waweze kutimiza malengo yao na ndoto zao za maisha. 

“Zingatieni elimu mnayopewa,hakikisheni mnaepuka vishawishi vinavyoweza kukatisha masomo yenu,mliopanga kwenye magheto msidhubutu kukaribisha wanaume kwenye magheto yenu lakini pia msiwafuate wanaume”,alieleza Maka. 

Kwa upande wake, Afisa mradi wa afya ya uzazi na ujinsia kwa vijana kutoka Shirika la Agape, Lucy Maganga alisema Kongamano hilo ni sehemu ya utekelezaji wa mradi huo unaofadhiliwa na Shirika la Kimataifa la Sida la nchini Sweden. 

Nao wanafunzi walioshiriki Kongamano hilo walieleza kufaidika kutokana na mradi huo kwani wamepata ujasiri wa kujieleza,kujitambua na kujithamini na kwamba kamwe hawawezi kushawishika kukatisha masomo kwa kupewa mimba wala kuolewa wakiwa katika umri mdogo. 

ANGALIA PICHA ZA MATUKIO HAPA CHINI 
Wanafunzi wa shule mbalimbali katika kata ya Usanda halmashauri ya wilaya ya Shinyanga wakiandamana kuelekea katika uwanja wa kijiji cha Singita kata ya Usanda ambapo pamefanyika kongamano kwa ajili ya kutoa elimu afya ya uzazi na ujinsia ili kutokomeza mimba na ndoa za utotoni. Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Wanafunzi wakiwa wameshikilia mabango wakiandamana kuelekea uwanjani.
Wanafunzi wakiwa wameshikilia bango wakati wa maandamano hayo.
Afisa mradi wa afya ya uzazi na ujinsia kwa vijana kutoka Shirika la Agape, Lucy Maganga akielezea lengo la kongamano la wanafunzi wa shule za msingi na sekondari kata ya Usanda ambalo limelenga kutoa elimu kuhusu afya ya uzazi na ujinsia ili .kukabiliana na mimba na ndoa za utotoni.
Kaimu Afisa Elimu wa Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga,Mary Maka akizungumza wakati wa Kongamano hilo na kuwataka wanafunzi kuzingatia masomo yao na kuepuka vishawishi vinavyoweza kukatisha masomo yao.
Kaimu Afisa Elimu wa Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga,Mary Maka akiwasisitiza wanafunzi/watoto kutoa taarifa kwa viongozi na vyombo vya dola pale wanapofanyiwa vitendo vya kikatili.
Afisa Maendeleo ya Jamii Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Aisha Omary akicheza na wanafunzi wakati wa kongamano hilo.
Afisa Maendeleo ya Jamii Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Aisha Omary akizungumza wakati wa kongamano hilo.
Meza kuu wakiwa katika uwanja wa kijiji cha Singita kata ya Usanda wakati wa kongamano hilo.
Wanafunzi wa shule ya sekondari Samuye wakionesha mchezo wa kuruka sarakasi.
Wanafunzi wa shule ya Sekondari Samuye wakitoa burudani. 
Wanafunzi wakifuatilia matukio mbalimbali yaliyokuwa yanaendelea.
Wanafunzi wakifuatilia matukio yaliyokuwa yanaendelea.
Wanafunzi wakiimba kwaya.

Awali Afisa mradi wa afya ya uzazi na ujinsia kwa vijana kutoka Shirika la Agape, Lucy Maganga akitambulisha wageni mbalimbali waliohudhuria kongamano hilo.
Mratibu wa  Mradi wa Afya ya Uzazi na Ujinsia - Save The Children Sweden unaofadhiliwa unaofadhiliwa na Shirika la Kimataifa la Sida la nchini Sweden,John Maliyapamba Komba ambaye ni Mtaalamu anayetoa msaada wa kitaalamu kwa asasi zinazotekeleza mradi wa wa Afya ya Uzazi na Ujinsia ambazo ni KIWOHEDE na Agape akizungumza wakati wa kongamano hilo.
Afisa Mtendaji wa kata ya Usanda Emmanuel Maduhu akizungumza wakati wa kongamano hilo na kuwasisitiza wanafunzi kuzingatia mambo wanayofundishwa shuleni.
Wanafunzi wakiendelea kutoa burudani ya nyimbo.
Mshereheshaji wakati wa kongamano hilo,Emmanuel Jonas akitoa maelekezo kabla ya kuanza kwa Mdahalo uliolenga kujadili Faida ya elimu ya afya ya uzazi na ujinsia kwa wanafunzi.
Mwanafunzi akieleza jinsi elimu ya afya ya uzazi na ujinsia ilivyomsaidia kujitambua na kujithamini.
Mwanafunzi akichangia hoja kuhusu faida ya elimu ya afya ya uzazi na ujinsia katika kukabiliana na mimba na ndoa za utotoni.
Mwanafunzi wa shule ya Sekondari Usanda Philipo Manjale akieleza namna wanavyotoa elimu kwa vijana wenzao kuhusu madhara ya kujihusisha na mapenzi katika umri mdogo.
Mwanafunzi wa shule ya sekondari Shingita,Davis Kafulila akichangia hoja kuhusu namna ya kukabiliana na mimba na ndoa za utotoni.
Mwanafunzi wa shule ya sekondari Samuye ,Joyce John akizungumza wakati wa mdahalo huo.Alisema watoto wengi wamekuwa wakijiingiza katika vitendo vya mapenzi kutokana na kukosa elimu kuhusu madhara ya kufanya mapenzi katika umri mdogo.
Wanafunzi na wazazi wakifuatilia mdahalo.
Mzazi,Amina Kushoka akichangia hoja wakati wa mdahalo.Aliwataka watu wazima kuacha kufuatilia watoto wadogo kwani wanawaharibia maisha huku akiwakumbusha wazazi wajibu wa kulea watoto wao kwa kukaa nao karibu ili wawaeleze changamoto wanazokutana nazo.
Musa Nangale,akichangia hoja.Aliwashauri wazazi kuepuka tabia ya kuozesha watoto wadogo.
Aziza Jumanne akizungumza wakati akiwakilisha kundi la wazee.Alisema hivi sasa jamii imeelimika na imepunguza vitendo vya kikatili dhidi ya watoto.
Wanafunzi wakiimba shairi.
Mwanafunzi wa shule ya sekondari Samuye akiimba wimbo wa Kufoka foka 'Rap'
Burudani ya ngoma ikiendelea wakati wa kongamano hilo.
Kongamano linaendelea.
Wakazi wa Usanda wakifuatilia matukio yaliyokuwa yanaendelea.
Kijana kutoka shule ya Sekondari Usanda akitoa burudani ya wimbo.
Wanafunzi wa shule ya sekondari Usanda wakiimba.
Mwakilishi wa dawati la jinsia na watoto Vivian Zabron akizungumza wakati wa kongamano hilo na kuwataka wanafunzi kutoa taarifa pale wanapobaini kuwepo kwa vitendo vya ukatili dhidi yao.
Muuguzi wa kituo cha Afya Usanda,Jesca Mabula akiwahamasisha wazazi na walezi kujenga urafiki na watoto na kuacha tamaa ya mali ili kukabiliana na ndoa na mimba za utotoni.
Walimu wa shule mbalimbali zilizopo katika kata ya Usanda wakifuatilia matukio yaliyokuwa yanaendelea.
Wanafunzi wakiwa kwenye kongamano hilo.
Wanafunzi wakionesha Igizo.
Wanafunzi wakiendelea kutoa burudani.
Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527