KIJANA AFARIKI AKIBATIZWA MTONI

Kijana mwenye umri wa miaka 20 amezama mtoni na kufariki wakati akibatizwa na mchungaji jijini Accra, Ghana.

Katika picha ya video ambayo imesambazwa kwenye mitandao ya kijamii, kijana huyo, Yaw Kyeremeh anaonekana akiwa katika kingo za Mto Densu akiwa akiwa na mchungaji ambaye alimzamisha majini.

Aliibuka baada ya kuzamishwa mara ya kwanza, na kufanyiwa maombi mafupi na kisha kuzamishwa kwa mara ya pili. Hakuibuka tena.

Msemaji wa jeshi la polisi jijini Accra, Afifa Tenge ameiambia BBC kuwa mchungaji msaidizi alikamatwa katika eneo la tukio huku msako mkali ukiendelea ili kumnasa mchungaji mkuu wa kanisa hilo.

Tukio hilo ambalo limetokea Jumapili limeibua hisia kali miongoni mwa wananchi wanaouliza iweje mtu apoteze maisha kwenye tukio la kidini.

Hata hivyo, familia ya Kyeremeh imenukuliwa na vyombo kadhaa vya habari nchini humo ikisema kuwa haimlaumu mtu yeyote kutokana na kifo cha mpendwa wao.

Kwa mujibu wa polisi mwili wa kijana huyo bado umehifadhiwa hospitali ukisubiri kufanyiwa uchunguzi kabla ya kukabidhiwa kwa familia ili uzikwe.

Picha ya video ya tukio hilo inaonesha kuwa baada ya kugundua kinachoendelea, mtu mmoja aliyekuwa karibuni alizamisha mkono wake majini ili kijana huyo aukamate na kujinasua.

Wakatai huo huo mchungaji aliyekuwa anaongoza ibada alionekana akihangaika kuogelea na kujinasua kutoka eneo hilo huku akipiga mayowe ya kuomba msaada.

Video ilikatika ghafla pale mtu ambaye alikuwa akirekodi alipoitupa simu yake ili kuongeza nguvu kwenye zoezi la uokoaji.

Sauti hata hivyo ziliendelea kusikika zikisema watu hao walionywa kuwa kina cha maji kimepanda kabla ya kuanza kwa ibada hiyo ya ubatizo.
Chanzo - BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527