Tanzia : ASKOFU EVARISTO CHENGULA AFARIKI DUNIA


Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linasikitika kutangaza kifo cha Askofu Evaristo Marcus Chengula wa Jimbo Katoliki la Mbeya kilichotokea, Jumatano, tarehe 21 Novemba 2018 majira ya saa 3:00 asubuhi kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Jijini Dar es Salaam. 

Akizungumza na Vatican News, Padre Charles Kitima, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania amesema, Marehemu Askofu Chengula aliwasili Jijini Dar es Salaam, Jumanne, tarehe 20 Novemba 2018 akiwa anasumbuliwa na ugonjwa wa moyo. 

Akapelekwa na kulazwa Muhimbili, jitihada za Madaktari kutaka kuokoa maisha yake, zikagonga mwamba na Askofu Evaristo Marcus Chengula akaaga dunia katika usingizi wa amani, akiwa na tumaini la ufufuko na maisha ya uzima wa milele!

Askofu Evaristo Marcus Chengula alizaliwa tarehe Mosi Januari 1941, huko Mdabulo, Wilaya y Mufindi, Mkoani Iringa. 

Baada ya masomo na majiundo yake ya kitawa na kipadre, tarehe 15 Oktoba 1970 akapewa Daraja Takatifu ya Upadre. 

Tarehe 8 Novemba 1996, Mtakatifu Yohane Paulo II akamteua kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Mbeya na kuwekwa wakfu kama Askofu tarehe 2 Februari 1997. 

Amefariki dunia akiwa amelitumikia Kanisa kama Padre kwa muda wa miaka 48 na Askofu kwa muda wa miaka 21!

 Apumzike katika usingizi wa amani, akiwa tayari kukutana uso kwa uso na Kristo Yesu, Hakimu mwenye huruma na mapendo!

Chanzo - Vatican News

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527