MKUU WA MKOA WA TABORA AWATAKA WAENDESHA BODABODA KUNUNUA PAFYUMU WATEJA WASHANGAE


Mkoa wa Tabora umejipanga kutoa huduma za uhakika pamoja na usalama katika kipindi cha siku tatu kuanzia leo Jumatano wakati wa jukwaa la fursa za uwekezaji na biashara linalotarajiwa kufunguliwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.

Akizungumza mjini Tabora Mkuu wa Mkoa huo, Aggrey Mwanri amewahakikishia wageni zaidi ya 500 watakaohudhuria watakuwa salama na kupewa huduma iliyo bora, na kusema tayari wamezungumza na watoa huduma ya usafiri wa bodaboda kuwa waaminifu kwa wateja wao pale watakaposahau mali zao.
Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri.

"Kwa wale watakaosahau mkoba kwenye bodaboda watajikuta wanapelekewa mikoba yao na waendesha bodaboda kwani hivyo ndivyo tulivyojipanga, pia nimezungumza na waendesha bodaboda kununua pafyumu kila mtu ili wateja wao washangae na kutoisahau Tabora" amesema Mwanri.

Mkuu huyo wa mkoa pia amewataka wananchi na wajasiriamali kuitumia fursa hiyo kikamilifu kujiongezea kipato ili kupambana na umaskini.
Chanzo - EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527